Dodoma Jiji FC yatangaza benchi la ufundi msimu wa 2025/2026

Na. Mussa Richard, DODOMA

Klabu ya Soka ya Dodoma Jiji FC, imemtambulisha Mashami Vicent raia wa Burundi kuwa kocha wake mkuu kuelekea kwenye msimu wa mashindano ya ligi kuu ya NBC msimu wa mwaka 2025/2026, sanjari na hilo imemtambulisha Bakira Guy raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuwa kocha msaidizi wa klabu hiyo.



Hayo yalibainishwa na Novatus John, Mtendaji Mkuu wa Dodoma Jiji FC, wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Vizano jijini Dodoma ukiwa na lengo la kutambulisha benchi jipya la ufundi.

“Baada ya kuvunja benchi letu zima la ufundi tulilokuwa nalo msimu uliopita, kama uongozi tulikaa chini na kuanza mchakato rasmi wa kutafuta benchi jipya la ufundi. Tulikuwa makini kupitia “CV” za makocha mbalimbali hatimae tukaweza kupata kocha bora zaidi ya wote na ndiye huyu ambaye tumemtangaza. Kwa upande wetu tutampatia stahiki zake zote ili timu yetu ifanye vizuri zaidi msimu ujao” alisema John.

Mashami Vicent kabla ya kutuwa Dodoma Jiji FC, alikuwa akiiongoza klabu ya Polisi FC, inayoshiriki ligi kuu nchini Burundi, akiisaidia timu hiyo kushinda makombe manne na kufanikiwa kuipeleka klabu hiyo kwenye mashindano ya shirikisho barani Afrika baada ya kupita miaka 10, pia amehudumu katika kikosi cha timu ya Taifa ya Burundi “Amavubi’’ kwa muda wa miaka minne.

Kuelekea msimu ujao wa mashindano Dodoma Jiji FC, itakita kambi jijini Arusha kwaajili ya kujiandaa na msimu mpya wa mashindano wa Ligi kuu ya NBC Tanzania bara, kambi hiyo inatarajia kuwa ya wiki tatu kuanzia Agosti 10, huku kambi hiyo ikilenga kuhusisha michezo mbalimbali ya kirafiki kwaajili ya kutafuta muunganiko wa timu, alisema.

Katika hatua nyingine Dodoma Jiji FC, inaendelea na zoezi la usajili ambapo mpaka sasa imekwisha watambulisha wachezaji mawili ambao ni Miraji Abdallah na kiungo Nelson Munganga. Alisema John.







Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Vijana waalikwa kushiriki Kongamano S/M Mbwanga