Wanawake watakiwa kulipa kodi na kukuza uchumi katika Jiji la Dodoma

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

Wanawake wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, hususan wafanyabiashara na wajasiriamali, wametakiwa kuendelea kulipa kodi na tozo kwa wakati ili kuchangia maendeleo ya jiji pamoja na kukuza uchumi wao na wa jamii kwa ujumla.



Wito huo ulitolewa na Diwani wa Viti Maalum Tarafa ya Zuzu, Pilly Hassan, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayotarajiwa kufanyika tarehe 8 Machi, 2026.

Alisema kuwa ulipaji wa kodi ni moja ya njia muhimu inayosaidia serikali  kupata mapato ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo kuboresha miundombinu ya masoko, barabara na huduma nyingine muhimu kwa wananchi. “Wanawake wengi wa Jiji la Dodoma tunajishughulisha na shughuli za biashara na ujasiriamali. Hivyo, tunapaswa kuwa mfano mzuri kwa kuhakikisha tunatimiza wajibu wetu wa kulipa kodi na tozo za serikali kwa hiari na kwa wakati. Kupitia kodi hii itaweza kutusaidia mambo mbalimbali na ya muhimu kama vile kujenga shule, masoko, barabara, hospitali na huduma nyingine. Hivyo, tunapaswa kuwa mstari wa mbele zaidi kuhakikisha jiji letu linakuwa kiuchumi kupitia mapato yetu” alisema Hassan.

Pia aliongeza kwa kusema “wanawake tunapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuchangia maendeleo ya jiji letu. Kupitia ulipaji wa kodi, tunasaidia kuimarisha uchumi wa jiji na pia kuendeleza biashara zetu na tuhakikishe tunahamasishana sisi kwa sisi katiia suala zima la ulipaji wa kodi” alisema Hassan.

Kwa upande wake, Diwani wa Viti Maalumu Tarafa ya Dodoma Mjini, Flora Liacho alisema kuwa wanawake wanapaswa kushirikiana na serikali katika nyanja mbalimbali. “Tunapaswa kuendelea kushirikiana na serikali katika kuibua fursa za kiuchumi pamoja na kuwahamasishana wanawake kujiunga katika shughuli za ujasiriamali zitakazowawezesha kujitegemea kiuchumi” alisema Liacho.



Lakini pia alitoa wito wanawake wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kujitokeza katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 8 Machi, 2026 ambapo kimkoa yatafanyika katika Wilaya ya Kongwa. “Nichukue fursa hii kuwataka wanawake wenzangu tuungane kwa pamoja katika siku yetu ya wanawake tujumuike kwenda kusheherekea katika Wilaya ya Kongwa, kuna vitu vingi vya kujifunza kama vile masuala ya ujasiliamali, haki kwa mwanamke na vitu vingine vingi. Hivyo, wanawake tujumuike kwa pamoja katika siku yetu” alisema Liacho.

Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani hufanyika kila mwaka tarehe 8 Machi na hulenga kuenzi mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii pamoja na kuhimiza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi na kijamii. Kwa mwaka 2026 Mkoa wa Dodoma unaadhimisha siku hiyo katika Wilaya ya Kongwa chini ya kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”.

Comments

Popular Posts

Mradi wa Maji Nala wa Bil. 1.3, mkombozi kwa wananchi

Jiji la Dodoma kuchangamkia fursa ujio wa Bandari Kavu Ihumwa