Wawezeshaji Stadi za Maisha watakiwa kuwa na nidhamu na uwajibikaji
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Wawezeshaji
wa Stadi za Maisha katika Shule za Sekondari Jiji la Dodoma wametakiwa kuwa na
nidhamu ya hali ya juu katika
mazingira ya shule watakazopangiwa pamoja na kutumia mafunzo waliyoyapata kwa
kuleta mabadiliko chanya kwa wanafunzi.
Hayo yalisemwa na Mwezeshaji mafunzo ya Stadi za Maisha wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Tuvacal Mjema, wakati wa mafunzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Dodoma jijini Dodoma.
Alisema
kuwa wawezeshaji wanapaswa kuwa mfano bora kwa wanafunzi kwa kuzingatia
maadili, kuwajibika ipasavyo na kuonyesha weledi katika utekelezaji wa majukumu
yao. “Ni
muhimu kwa wawezeshaji kuwa na nidhamu ya hali ya juu wanapokuwa shuleni.
Tunapaswa kuishi yale tunayowafundisha wanafunzi ili waweze kutuamini na
kufuata miongozo tunayowapatia kwasababu ninyi ndio taa yao inayo waangazia” alisema Mjema.
Lakini
pia aliongezea kwa kusema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwaongezea uwezo wa
kitaaluma na kisaikolojia wawezeshaji ili waweze kuwasaidia wanafunzi. “Kupitia mafunzo haya
ninaamini kuwa tunawaongezea walimu ujuzi ili kuweza kukabiliana na changamoto
mbalimbali za wanafunzi zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku na masomo
kwa ujumla” alisema Mjema.
Kwa upande wake, Sophia Kasekwa ambaye ni Mwezeshaji wa Stadi za Maisha katika Shule ya Sekondari Miyuji, alisema kuwa kupitia mafunzo hayo wamepata maarifa na mbinu zitakazowawezesha kuwafikia wanafunzi kwa ufanisi zaidi. “Tunashukuru kwa fursa hii ya mafunzo. Yametupa mwanga mpana wa namna ya kuwasaidia wanafunzi, hasa wale wenye changamoto mbalimbali za kimaadili, kisaikolojia na kijamii. Pia, kupitia elimu ya stadi za maisha, wanafunzi watajengewa uwezo wa kufanya maamuzi sahihi, kujiamini na kukabiliana na shinikizo rika, hali itakayochangia kuboresha taaluma na mwenendo wao shuleni na katika jamii kwa ujumla” alisema Kasekwa.
Mafunzo
hayo yanatarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika Shule za Sekondari
jijini Dodoma, lakini pia kuwajengea wanafunzi maarifa, ujuzi na mitazamo
chanya itakayowawezesha kujitambua, kujiamini, kufanya maamuzi sahihi na
kukabiliana kwa ufanisi na changamoto za maisha ya kila siku, ili waweze kuwa
raia wenye maadili mema, uwajibikaji na mchango chanya katika jamii na taifa
kwa ujumla.
MWISHO
Comments
Post a Comment