Stadi za Maisha Kuwa mkombozi kwa wanafunzi wa Sekondari jijini Dodoma
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Elimu
ya Stadi ya Maisha imetajwa kuwa ni chachu ya mabadiliko chanya kwa wanafunzi katika
kuwajengea uwezo wa kujitambua na kukabiliana na changamoto za maisha katika shule
za sekondari jijini Dodoma.
Hayo aliyasema Afisa Elimu Sekondari wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Daniel Mapilya wakati akifungua mafunzo kwa wawezeshaji wa stadi za maisha katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Dodoma.
Alieleza
kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuhakikisha wawezeshaji wanapata uelewa wa
kutosha juu ya namna bora ya kuwafikia wanafunzi na kuwajengea misingi imara ya
maisha. “Tunapozungumzia stadi za maisha, tunalenga kumsaidia mwanafunzi
kujitambua, kujiamini na kufanya maamuzi sahihi. Elimu hii itawawezesha vijana
wetu kuepukana na vishawishi vinavyoweza kuathiri masomo na mustakabali wa
maisha yao” alisema Mapilya.
Aliongeza
kwa kusema kuwa changamoto nyingi zimekuwa zikiwakumba watoto wa kike. ”…zikiwemo
shinikizo la rika na mazingira yasiyo rafiki, hivyo elimu hiyo itawapa ujasiri
wa kusimamia ndoto zao na kupambana na hali yoyote inayoweza kuwakwamisha, na kuweza
kuwajengea wanafunzi uwezo wa kusema hapana na kusimamia maamuzi yao ni sehemu
muhimu ya kuwapa kinga dhidi ya changamoto za kijamii” alisema Mapilya.
Kwa
upande wake, mwezeshaji wa mafunzo hayo, Lauden Emanuel, alisema kuwa mafunzo ya
stadi za maisha ni nyenzo muhimu katika kumlea kijana mwenye malengo na maadili.
“Tunataka kuona wanafunzi wanajijengea uwezo wa kufikia ndoto zao. Kupitia
stadi za maisha, tutawasaidia hasa wanafunzi wa kike kujiamini, kujitambua na
kusimama imara katika kufanikisha malengo yao ya elimu na maisha kwa ujumla. Kupitia
mafunzo haya wanafunzi watajifunza namna ya kupanga malengo yao, kuyafuatilia
na kuyatimiza kwa nidhamu na bidii” alisema Emanuel.
Wawezeshaji waliopatiwa mafunzo hayo wanatarajiwa kuwa daraja muhimu la kufikisha maarifa kwa wanafunzi, hatua itakayosaidia kuongeza ufaulu, kuimarisha nidhamu na kujenga kizazi chenye maadili na uwezo wa kukabiliana na changamoto za dunia ya sasa.
MWISHO
Comments
Post a Comment