Utatuzi mgogoro wa Mahomanyika watangazwa
Na.
Nancy Kivuyo,
NZUGUNI
Wizara
ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeunda timu mbili ya wataalam wa
upangaji na upimaji na timu ya uhakiki kwaajili ya kutatua mgogoro wa ardhi wa
muda mrefu katika eneo la Mahomanyika.
Timu hizo zimeundwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo alipokuwa akihutubia mamia ya wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika eneo la Mahomanyika, Kata ya Nzuguni jijini Dodoma.
Alisema
kuwa timu hizo zitaanza kazi mara moja ili kuhakikisha zoezi hilo linakamilika
kwa wakati. “Eneo la Mahomanyika ni la serikali kwahiyo, naagiza lipangwe na kupimwa
kwaajili ya kutatua mgogoro huu na kuwa kielelezo cha utatuzi wa migogoro
mingine iliyopo ndani ya Jiji la Dodoma. Timu hizi zinapaswa kufanya kazi ndani
ya siku 60 na kukamilisha zoezi hili ili kila mmoja ajue amepata nini na
anaenda wapi” alisema Dkt. Akwilapo.
Aliongeza kuwa wale wote waliohusika kwenye kadhia ya
mgogoro huo wa ardhi watachukuliwa kwaajili ya mahojiano ili wakatoe maelezo ya
kina ya kuwezesha suluhu kupatikana. “Wale wote ambao kwa namna moja au
nyingine walihusika kwenye kadhia hiyo watatafutwa na watahojiwa ili sasa watoe
maelezo yatakayosaidia kupatikana suluhu ya mgogoro kwasababu tunataka suala
hili liishe na maisha mengine yaendelee” aliongeza Dkt. Akwilapo.
Alimalizia kwa kutoa rai kwa viongozi wa ngazi zote za mitaa, kata na vitongoji kutambua kuwa masuala ya ardhi yanahitaji utaalam na nidhamu huku akikemea tabia ya viongozi kujifanya wamiliki wa ardhi na kusisitiza kuwa ili nchi iendelee, inahitaji mambo manne ambayo ni watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora na kwamba uongozi bora unajumuisha weledi katika kusimamia ardhi.
Katika hatua nyingine, Diwani wa Kata
ya Nzuguni, Leonard Ndama, aliushukuru ujio wa waziri na timu yake akisema kuwa
anatarajia mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu utamalizwa na hatimae wananchi
kupata kile wanachostahili. “Nakushukuru sana Mheshimiwa waziri na jopo lote
hili kwa kufika hapa Mahomanyika, ninaamini ya kuwa ujio wenu ni kusudi tosha
la kupata majibu ya mgogoro huu na kufikia tamati kwa changamoto hii
kutatuliwa” alisema Ndama.
Mgogoro huo unahusisha Mtaa wa
Mahomanyika (Kata ya Nzuguni) na Mitaa ya Azimio na Sokoine (Kata ya Ipala)
ambapo eneo lenye mgogoro lina jumla ya ekari 4,363. Hapo awali, mwaka 1976
eneo hilo lilipangwa kuwa "Green Belt" yaani Ukanda wa Kijani. Mpango
wa mwaka 2019-2040 ulibadilisha matumizi hayo kuwa "Urban Farming" yaani
Mashamba ya Mjini ambapo mwaka 2022, Jiji la Dodoma lilipanga viwanja 1,990
katika eneo hilo, hali iliyozua malalamiko kutoka kwa wananchi waliodai kuwa
wamiliki wa asili.
MWISHO
Comments
Post a Comment