Msalala DC wajifunza mbinu za ukusanyaji mapato kupitia mfumo wa kanda Dodoma Jiji

Na. Mwandishi Wetu

Halmashauri ya Wilaya ya Msalala imetembelea Ofisi ya utoaji huduma Kanda Namba Moja iliyopo Soko la wazi la Machinga, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, ili kujifunza mbinu za ukusanyaji wa mapato kupitia mfumo wa kanda ambao umesaidia kuongeza ufanisi wa makusanyo na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.


Akielezea namna ya utendaji kazi wa kanda hiyo, Nicholaus Mitembo, Meneja wa Kanda Namba Moja, alisema kuwa kanda hiyo inatoa elimu kwa wananchi na wafanyabiashara na kuwahamasisha kulipa mapato kwa hiari na kwa wakati ili kuepuka adhabu na pia kuchangia maendeleo ya eneo lao. Aidha, alisema kanda hiyo inatarajia kukusanya mapato ya shilingi 19,162,421,314.32.

Nae, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Msalala, Rose Manumba, aliishukuru Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kukubali na kutoa nafasi ya kujifunza katika halmashauri hiyo. Aidha, aliwakaribisha viongozi na watumishi wa jiji hilo kutembelea Msalala kwa ajili ya kujifunza zaidi kuhusu shughuli kuu za kiuchumi za eneo hilo, ambazo ni uchimbaji madini na kilimo.

Mhasibu wa Mapato wa Halmashauri ya Wilaya ya Msalala, Kidana Milando, alisema kuwa lengo la ziara hiyo lilikuwa kujifunza mbinu mbalimbali zitakazosaidia kuongeza bajeti ya halmashauri kutoka shilingi bilioni saba hadi bilioni tisa, hususan kutoka maeneo yanayofanya vizuri ndani ya kanda, ili kupata uzoefu na maarifa yatakayosaidia kuboresha utendaji na utekelezaji wa majukumu katika halmashauri yao.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mwalugulu, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala, Frola Sagasaga, alisema kuwa walifika kwa lengo la kujifunza kuhusu masuala ya ukusanyaji wa mapato. Alifafanua kuwa mwenyekiti wao aliwashauri kutembelea Jiji la Dodoma kutokana na mafanikio yake katika ukusanyaji wa mapato kupitia kanda, akibainisha kuwa jiji hilo linafanya vizuri zaidi katika eneo hilo.

Ziara hiyo imeelezwa kuwa imewapa madiwani na wataalamu wa Halmashauri ya Wilaya ya Msalala uzoefu na maarifa mapya yatakayowasaidia kuboresha mifumo ya ukusanyaji wa mapato, kwa lengo la kuongeza ufanisi na kufikia malengo ya bajeti ya halmashauri yao.

MWISHO

Comments