Jiji la Dodoma latumia Mil. 29 miundombinu S/M Ihumwa B
Na. Mwandishi Wetu, IHUMWA
Halmashauri ya Jiji la
Dodoma imetoa kiasi cha shilingi 29,000,000 kwaajili ya umaliziaji wa vyumba
vitatu vya madarasa ya Shule ya Msingi Ihumwa B, hatua inayosaidia kuimarisha
mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia.
Hayo aliyasema Mwalimu
Mkuu wa Shule ya Msingi Ihumwa B, Mwl. Daudi Mwakalinga wakati alipokuwa
akisoma taarifa mbele ya Kamati ya Fedha na Utawala ya Halmashauri ya Jiji la
Dodoma iliyoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Elimu na Afya katika
ziara ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo kwa robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha
2025/2026.
Alisema kuwa fedha hizo zilipeleka
mabadiliko chanya shuleni hapo. “Kupitia fedha hizi, shule imefanikiwa
kuboresha madarasa, hali iliyochangia kuongeza hamasa kwa walimu na wanafunzi
katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji” alisema Mwl. Mwakalinga.
Pia, alitoa shukrani kwa
Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kuwapatia fedha hizo kwa ajili ya kuboresha
miundombinu ya shule. “Tunatoa shukrani za dhati kwa uongozi Jiji kwa kutupatia
fedha hizi ambazo zimekuwa chachu ya maendeleo katika shule yetu. Mazingira ya
sasa ni rafiki zaidi kwa walimu na wanafunzi” alishukuru Mwl. Mwakalinga
Kwa upande wake,
Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Elimu na Afya, Joan Mazanda alitoa pongezi kwa
uongozi wa shule hiyo, hususan kwa Mwalimu Mkuu kwa usimamizi mzuri wa
utekelezaji wa miradi ya maendeleo. “Usimamizi huu umeonesha matumizi sahihi ya
fedha za umma na kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa viwango vinavyokubalika. Pia
nipende kusisitiza kuendelea kudumisha uwajibikaji katika miradi ambayo
inatekelezwa na serikali” alisema Mazanda.
Fedha za mapato ya ndani
zinazotolewa kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji zinachangia
kuinua kiwango cha elimu katika miradi yote inayotekelezwa na Halmashauri ya
Jiji la Dodoma hivyo kuboresha kiwango cha elimu ya mtu mmoja mmoja na jamii
nzima kwa ujumla.
MWISHO
Comments
Post a Comment