Mwalimu Mkuu S/M Mazengo apongezwa usimamizi ukarabati wa shule
Na. Dennis Gondwe, KIKUYU KASKAZINI
Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma
imempongeza Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mazengo kwa kusimamia vizuri
ukarabati wa shule kupitia fedha za mradi wa BOOST na kumtaka kuongeza kasi
kukamilisha kabla ya shule kufunguliwa ili wanafunzi wasiwe na upungufu wa
madarasa ya kusomea.
Pongezi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipoongoza timu hiyo kukagua ukarabati wa shule hiyo jijini Dodoma.
Baada ya kupokea taarifa ya ukarabati wa shule hiyo
iliyowasilishwa kwa ustadi na mwalimu mkuu na kukagua mradi huo, Mwenyekiti wa
Timu ya Menejimenti alisema kuwa mwalimu mkuu (Mwl. Rehema Nkungu) anafanya
kazi kubwa na nzuri ya kusimamia ukarabati wa mradi huo. “Hapa kuna ushirikiano
mzuri, ninataarifa ya utendaji mzuri wa (Mkaguzi Majengo, Jacob Stephen)
anayesimamia mradi huu tangu nikiwa ofisini, hongera sana. Matamanio yetu, kasi
iongezeke ya ukarabati huu ukamilike haraka ili wanafunzi wanapofungua wakute
ukarabati umekamilika” alisema Dkt. Sagamiko.
Akielezea utekelezaji wa mradi huo, Mwalimu Mkuu wa
Shule ya Msingi Mazengo, Mwl. Rehema Nkungu alisema kuwa shule yake ilipokea
shilingi 170,400,000 kwa ajili ya ukarabati wa shule na ujenzi wa matundu 12 ya
vyoo fedha kutoka mradi wa BOOST. “Shilingi 150,000,000 ni fedha ya ukarabati
wa madarasa 13 na shilingi 20,400,000 kwa ajili ya ujenzi wa matundu 12 ya
vyoo” alisema Mwl. Nkungu.
Alisema kuwa malengo ya ukarabati huo ni kuboresha
miundombinu ya madarasa kwa ajili ya matumizi salama. “Kurejesha ubora wa
majengo yaliyoharibika na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma ya elimu kupitia
mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia” alisema Mwl. Nkungu.
Shule ya Msingi Mazengo ilianza tarehe 1 Januari, 1970
hadi sasa ina wanafunzi 720, kati yao wavulana ni 324 na wasichana 396.
MWISHO
Comments
Post a Comment