Diwani Iyumbu apongezwa usimamizi miradi

Na. Dennis Gondwe, IYUMBU

DIWANI wa Kata ya Iyumbu amepongezwa kwa kusimamia miradi ya maendeleo na kutakiwa kuendelea kutoa ushirikiano kwa wataalam wa kata hiyo ili kukamilisha miradi kwa wakati ili iweze kutoa huduma kwa wananchi.


Pongezi hizo zilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipoongoza Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji kutembelea na kukagua ukamilishaji wa madarasa mawili, maabara tatu, jengo la utawala na matundu nane ya vyoo katika Shule ya Sekondari Iyumbu.

“Mheshimiwa Diwani ninakupongeza kwa kusimamia vizuri miradi katika Kata ya Iyumbu. Kwa umoja huu kata inakwenda kubadilika kimaendeleo, wape ushirikiano wataalam katika kata ili kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kwa nafasi yako upo katika wakati mzuri zaidi kuhamasisha wananchi kujitolea kushiriki shughuli za maendeleo na nguvu kazi” alisema Dkt. Sagamiko.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Iyumbu, Sadick Mpondamali aliishukuru halmashauri kwa kutoa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuahidi kusimamia vizuri matumizi ya fedha hizo.

Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Ugavi, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Vincent Odero alisema kuwa kwa mujibu wa mpango kazi wa utekelezaji wa mradi, vifaa vinatakiwa kuwa eneo la mradi angalau siku saba kabla ya kazi husika ili kutokusababisha mkwamo wa kazi.

Awali akiikaribisha Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Kaimu Mkuu wa Divisheni ya Elimu Sekondari, Mwl. Fredrick Mwakisambwe aliwataarifu kuwa shule hiyo ilipokea shilingi 168,000,000 kwa ajili ya ukamilishaji wa madarasa mawili, maabara tatu, matundu nane ya vyoo na jengo la utawala fedha kutoka mapato ya ndani ya halmashauri.





MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma