Menejimenti ya Jiji la Dodoma yaelekeza ukarabati S/M Dodoma Mlimani kufanyika usiku na mchana
Na. Dennis Gondwe, TAMBUKARELI
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Dodoma Mlimani
ametakiwa kusimamia ukarabati wa madarasa 12 kufanyika hadi usiku ili ukamilike
mapema kabla ya shule kufunguliwa kwa sababu fedha shilingi 150,000,000
zimeshatolewa.
Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipoongoza Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kutembelea na kukagua maendeleo ya ukarabati wa madarasa 12 kwa shilingi 150,000,000 fedha kutoka mradi wa BOOST.
Alisema kuwa kazi ya ukarabati inatakiwa kufanyika
usiku na mchana ili kukamilisha madarasa hayo kwa wakati. Aliongeza kuwa fedha
ipo, hivyo, hakuna sababu ya kufanya mradi uchelewe kukamilika, na kuwataka
afisa mtendaji kata na mtaa kuweka kambi shuleni hapo kusimamia utekelezaji wa
ukarabati wa shule hiyo.
Akiongelea mradi huo, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi
Dodoma Mlimani, Mwl. Jenipher Mhavile alisema kuwa ukarabati ulianza 13 Oktoba,
2025. “Hatua ya ukarabati hadi tarehe 24 Desemba, 2025 madarasa yote 12 yapo
hatua ya upauaji na kuweka mbao za kupokea gypsum board na uwekaji wa fremu za
milango” alisema Mwl. Mhavile.
Shule ya Msingi Dodoma Mlimani ilianza mwaka 1974, na
sasa ina jumla ya wanafunzi 672.
MWISHO
Comments
Post a Comment