Jiji lataka mpango kazi kukamilisha ujenzi shule ya Mil. 299,200,000 utekelezwe
Na. Dennis Gondwe, NZUGUNI
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imemuagiza Mkuu wa Shule
ya Sekondari Nzuguni kusimamia mpango kazi wa ujenzi wa shule mpya ya msingi ya
mkondo mmoja yenye gharama ya shilingi 299,200,000 fedha kutoka mradi wa BOOST
ili ikamilike kwa wakati kwa mujibu wa mkataba.
Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipoongoza timu hiyo kutembelea na kukagua hatua ya ujenzi wa shule hiyo katika Kata ya Nzuguni, jijini Dodoma.
Alisema kuwa mpango kazi wa ujenzi wa shule hiyo
unatakiwa kufahamika na kila anayehusika na kusimamia utekelezaji wake ili
ujenzi ukamilika kwa wakati. Idadi ya mafundi anatakiwa kuongezeka ili
kuhakikisha mradi unakamilika haraka, aliongeza.
Pia, ilishauriwa manunuzi yote ya vifaa pamoja na
madawati yatangazwe kwenye mfumo wa NeST mapema ili kusiwe na ucheleweshaji
katika utekelezaji wa mradi.
Akiwasilisha taarifa ya ujenzi wa shule mpya ya msingi
mkondo mmoja kwa Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mkuu wa
Shule ya Sekondari Nzuguni, Mwl. Rogers Justinian alisema kuwa shule ilipokea
shilingi 299,200,000 fedha kutoka mradi wa BOOST. Ujenzi unaotekelezwa ni jengo
la utawala, madarasa sita ya msingi, madarasa mawili ya awali, matundu 12 ya
vyoo vya msingi na matundu sita ya vyoo vya awali, alisema.
Alisema kuwa ujenzi uliganywa katika ‘lots’ sita ili
kupata mafundi sita, kwa madarasa mawili kila ‘lot’, jengo la utawala na vyoo.
Hatua iliyofikiwa ni upauaji kwa madarasa manne na vyoo, majengo mengine yapo
kwenye hatua ya lenta.
Akiongelea matumizi ya fedha alisema kuwa shilingi
125,678,528 zilitumika kulipa wazabuni na mafundi, bakaa ni shilingi 176,521,472.
MWISHO
Comments
Post a Comment