Jiji la Dodoma lataka kasi ukarabati madarasa Kitelela Sec
Na. Dennis Gondwe, NZUGUNI
TIMU ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma
imeelekeza kuongeza kasi ya ukamilishaji wa ukarabati wa madarasa mawili katika
Shule ya Sekondari Kitelela ili wanafunzi watakapofungua shule mwezi Januari,
2026 waweze kuyatumia.
Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipoongoza timu hiyo kutembelea na kukagua maendeleo ya ukamilishaji wa ukarabati wa madarasa mawili katika Shule ya Sekondari Kitelela iliyopo Kata ya Nzuguni, jijini Dodoma.
Dkt. Sagamiko ambae ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji
la Dodoma alisema kuwa baada ya kukagua hali ya ukarabati inavyoendelea, kasi
siyo ya kuridhisha. “Hivyo, maelekezo yetu ni kwamba, kasi iongezeke ili mradi
ukamilike kwa wakati na shule zinapofunguliwa wanafunzi waanze kutumia madarasa
hayo” alisema Dkt. Sagamiko.
Wakati huohuo, alimuagiza Afisa Mtendaji wa Kata ya Nzuguni
na Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Kitelela kuweka kambi katika mradi huo na
kusimamia ratiba ya utekelezaji na kuhakikisha changamoto zinapatiwa ufumbuzi
ikiwemo ya upatikanaji wa maji.
Vilevile, mkuu wa shule aliagizwa kusimamia
menejimenti ya vifaa vinavyonunuliwa, kupokelewa na kutolewa kwa ajili ya
shughuli za ukarabati na kusisitiza utunzaji sahihi wa kumbukumbu. “Hapa,
daftari la mali za serikali au kitabu cha kumbukumbu za mali za serikali lazima
kitumike vizuri kuandika orodha ya mali na vifaa vyote vya serikali vinavyonunuliwa
kwa ajili ya kazi ya ukarabati” alisema Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Ugavi,
Vincent Odero.
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi wa
ukamilishaji wa ukarabati wa vyumba viwili vya madarasa na ofisi, Mkuu wa Shule
ya Sekondari Kitelela, Mwl. John Mswelo alisema kuwa shule hiyo ilipokea fedha
tarehe 18 Novemba, 2025 kupitia akaunti ya Shule ya Sekondari Nzuguni B kwa
ajili ya ukamilishaji wa madarasa mawili na ofisi, ujenzi ulianza tarehe 11
Desemba, 2025.
Akiongelea utekelezaji wa mradi, alisema kuwa kazi
zilizofanyika ni upigaji lipu kuta za ndani na nje na ‘blundering’ ndani ya
jengo. “Kazi zilizobaki ni ‘blundering’ sehemu ya nje, kufunga bodi katika
dari, kupaka rangi, kuweka mfumo wa umeme, uwekaji wa milango na uwekaji wa
marumaru katika sakafu. Kiasi cha shilingi 6,865,830 kimetumika kwa ajili ya
manunuzi ya vifaa awamu ya kwanza” alisema Mwl. Mswelo.
Awali akiikaribisha Timu ya Menejimenti ya Halmashauri
ya Jiji la Dodoma katika eneo la mradi, Kaimu Mkuu wa Divisheni ya Elimu
Sekondari, Mwl. Fredrick Mwakisambwe alisema kuwa halmashauri ilitoa kiasi cha
shilingi 20,7743,095 kwa ajili ya kukamilisha mradi kiporo wa madarasa mawili
na ofisi katika Shule ya Sekondari Kitelela.
Shule ya Sekondari Kitelela ipo kilometa 22 kutoka
katikati ya Jiji la Dodoma, ilifunguliwa tarehe 13 Januari, 2025 ikiwa na
wanafunzi 31 na inatarajia kupokea wanafunzi 21 wa kidato cha kwanza mwaka
2026.
MWISHO
Comments
Post a Comment