Chidachi S/M watakiwa kuboresha mpango kazi wa fundi kukamilisha ujenzi mradi wa BOOST

Na. Dennis Gondwe, MKONZE

Mhandisi wa halmashauri, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Chidachi wametakiwa kufanya mapitio ya mpango kazi wa mafundi na kuandaa mpango wa haraka unaotekelezeka ili kukamilisha mradi wa ujenzi wa miundombinu kwa gharama ya shilingi 182,100,000 fedha kutoka mradi wa BOOST shuleni hapo.


Agizo hilo lilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipoambatana na Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kukagua ujenzi wa mradi wa miundombinu katika Shule ya Msingi Chidachi kwa fedha za ufadhili wa BOOST.

Timu ya Menejimenti ilipokagua mradi huo haikuridhika na kasi ya ujenzi na kuelekeza mhandisi wa halmashauri, mwalimu mkuu pamoja na fundi kupitia upya mpango kazi na kutengeneza mpango kazi wa haraka unaotekeleza ili kukamilisha mradi huo kwa wakati uliopangwa.

Mkurugenzi alisema kuwa kila mmoja anatakiwa kuongeza umakini katika usimamizi ili mradi ukamilishwe kwa viwango, na kusema kuwa menejimenti haitachelewesha malipo ya fundi kwa namna yeyote.

Akisisitiza katika utekelezaji wa mradi huo, alisema kuwa ujenzi wa madarasa uende sambamba na ununuzi wa madawati na ujenzi wa jengo la utawala uende sambamba na ununuzi wa samani. “Nimesisitiza haya kwa sababu hakuna fedha itakayoongezwa kwenye mradi huu kwa ajili ya samani” alisema Dkt. Sagamiko.

Katibu wa Kamati ya Ujenzi, Mwl. Veronica Suya alisema kuwa shule ilipokea shilingi 182,100,000 kutoka mradi wa BOOST kwa ajili ya ujenzi wa madarasa mawili ya awali na matundu sita ya vyoo, madarasa mawili ya elimu msingi na jengo la utawala. “Utekelezaji wa mradi huu ulianza tarehe 23 Septemba, 2025. Mradi unalenga kupunguza msongamano wa wanafunzi na kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi” alisema Mwl. Suya.

Shule ya Msingi Chidachi ipo katika Mtaa wa Chidachi, Kata ya Mkonze ilianzishwa tarehe 3 Aprili, 2004. Shule ina wanafunzi 1,717 na walimu 50.






MWISHO

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma