Vijana watakiwa kuchangamkia fursa mbalimbali ili kujikwamua kiuchumi
Na. Leah Mabalwe, MNADANI
Mwakilishi wa Kampuni ya MAINLAND inayojenga Kiwanda
cha kutengeneza mafuta ya Alizeti, Fadhili Makenjula awataka vijana kujitokeza
katika nafasi za kazi mbalimbali zitakazotangazwa na kiwanda hicho cha Mafuta
kitakapo kamilika mwezi Juni, 2025 ili kujikwamua kiuchumi.
Mwakilishi wa Kampuni ya MAINLAND inayojenga Kiwanda cha kutengeneza mafuta ya Alizeti, Fadhili Makenjula |
Aliyazungumza hayo kwenye Kongamano la Vijana katika Mbio za Mwenge wa Uhuru Mwaka 2025 lililofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Mbwanga jijini Dodoma.
Alisema kuwa vijana wanapaswa kuchangamkia fursa bila
kuchagua kazi ili kujikwamua kiuchumi. “Nipende kuwataarifu kuwa, tupo katika
hatua ya umaliziaji wa ujenzi wa kiwanda kikubwa cha mafuta ya alizeti kilichopo
Kata ya Msalato, Mtaa wa Veyula. Vijana jitokezeni kwa wingi katika kutuma
maombi ya kazi, kuna vitengo mbalimbali katika kiwanda hicho. Wewe kama kijana
usiogope kuleta maombi yako kwaajili ya nafasi ya kazi. Tunawapa vijana nafasi
kubwa kwasababu nyie ndio wajenzi wa taifa hili” alisema Makenjula.
Kwa upande wake Mhadhiri Ndaki ya Sayansi, Siasa na
Utawala wa Umma katika Chuo kikuu cha Dodoma, Dkt. Pius Nyamhanga aliwataka vijana
kujitokeza na kushiriki katika fursa mbalimbali za kazi zitakazo jitokeza. Alisema
kuwa kizazi hiki kimepata bahati ya kushuhudia mageuzi ya kimaendeleo katika
sekta zote. “Vijana wote muwe tayari kujitokeza katika fursa za kazi na muwe mstari
wa mbele na tayari kufanya kazi kwa mazingira yanayowazunguka. Fursa nyingi
huwa zinatokea mlipo na mara nyingi fursa hizo zinawalenga hasa vijana kama
mlivyosikia hapa kuwa kuna nafasi za kazi katika kiwanda kipya cha mafuta ya
alizeti. Hivyo, msibaki nyuma na muwe mstari wa mbele kupitia fursa hiyo”
alisema Dkt. Nyamhanga.
Alimalizia kwa kusema “niwaombe sana wazazi muwe mstari wa mbele katika kuwaelimisha watoto wenu kuzifahamu fursa mbalimbali za kazi. Pia mnawajibu wa kukaa na kuwashauri vijana wenu kutochagua kazi. Mnamchango mkubwa wa kuwapa darasa la maisha vijana wetu hawa” alimalizia Nyamhanga.
MWISHO
Comments
Post a Comment