Mzee Bukitu aongelea Falsafa ya Mwenge wa Uhuru kwa Vijana Dodoma

Na. Nancy Kivuyo, MNADANI

Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation, Mzee Joseph Butiku amesema falsafa ya Mwenge wa Uhuru ilianzishwa kwa lengo la kuleta upendo na mshikamano kwa taifa huku mwanga wa Mwenge ukiangazia mipaka ili kuleta matumaini palipo kukata tamaa, upendo palipo uadui na heshima palipo chuki.



Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation, Mzee Joseph Butiku akielezea Falsafa ya Mwenge wa Uhuru

Aliyasema hayo katika Kongamano la Mwenge wa Uhuru la Vijana 2025 lililofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Mbwanga. Alisema kuwa katika kipindi cha mwaka 1958 Mwalimu Nyerere alianzisha falsafa hiyo kipindi cha jitihada za kupata uhuru. “Niwaeleze kuwa, Mwenge wa Uhuru ni kielelezo cha amani na matumaini. Wakati sisi tunapata ufahamu kuhusu Mwenge, tuliingiwa na uzalendo wa hali ya juu ndio maana mnaona taifa letu lipo imara hadi leo” alisema Mzee Butiku.

Aliongeza kuwa vijana wa kizazi cha leo wanapaswa kuisoma historia ya Mwenge wa Uhuru kwa mapenzi ya dhati ili kuukuza uzalendo wao na kudumisha amani ya nchi. “Vijana mlioshiriki kongamano hili nawapongeza sana kwasababu mnajifunza na kujikumbusha mambo muhimu kwa ajili ya mustakabali wa maisha yenu na ya taifa letu. Nawasihi muendelee na juhudi hizi na mkawe mabalozi kwa vijana wenzenu ili kuienzi historia ya Mwenge wa Uhuru kwa uaminifu mkubwa” aliongeza Mzee Butiku.

Nae Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma Ndaki ya Sayansi, Siasa na Utawala wa Umma, Justine Kajerero alisema kuwa falsafa ya mbio za Mwenge wa Uhuru, uadilifu na uongozi vinachochea uzalendo wa kweli wa kuipenda nchi. “Dhana ya uadilifu ni hali ya kufanya jambo kwa usahihi hata kama kuna mwanya wa kufanya vingenevyo. Vijana tumeaminiwa sana na serikali yetu, leo kuwepo mahali hapa kujadili mambo muhimu kama uadilifu na uongozi ni jambo kubwa litakaloleta matokeo chanya miongoni mwetu” alisema Kajerero.


Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma Ndaki ya Sayansi, Siasa na Utawala wa Umma, Justine Kajerero

Aliongeza kuwa mustakabali wa kuijenga nchi imara yenye vijana waadilifu na viongozi bora upo mikononi mwa vijana. “Niwaambie kwamba vijana waadilifu wanaandaliwa tangu sasa, tuhudhurie mijadala ya kujenga ili kuongeza maarifa na uzalendo kwaajili ya kuuimarisha umoja, upendo na heshima ya nchi yetu” alisisitiza Kajerero.

Katika hatua nyingine, mwananchi wa Kata ya Mnadani, Julius Mtemi alisema kuwa amefurahi kushiriki kongamano hilo na amejifunza mambo mengi ikiwemo umuhimu wa Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Mzee Joseph Butiku. “Kiukweli leo nimepata maarifa mengi, yamenijenga na natumaini nitaenda kuwaeleza jamaa zangu ili nao wajue umuhimu wa mwenge na uzalendo wa kweli” alisema Mtemi.




Kongamano la Mwenge wa Uhuru la Vijana Mwaka 2025 ni la pili kufanyika katika Wilaya ya Dodoma na limewakutanisha vijana 950 waliojadili fursa za kiuchumi kwa vijana, masuala ya afya na afya ya uzazi na makuzi ya vijana, uongozi, uadilifu, uzalendo kwa taifa na falsafa ya mbio za Mwenge wa Uhuru, kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa amani na utulivu na stadi za kazi na stadi za maisha kwa vijana.

MWISHO       

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo