Mwenge wa Uhuru kutembelea miradi 7 ya shilingi Bil. 11.1 Dodoma

Na. Dennis Gondwe, CHIGONGWE

MWENGE wa Uhuru Mwaka 2025 utatembelea miradi saba ya maendeleo yenye gharama ya shilingi bilioni 11.1 iliyotekelezwa kwa ajili ya kuwapelekea maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi katika Wilaya ya Dodoma.


Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri (kushoto) wakati akipokea Mwenge wa Uhuru Mwaka 2025 kutoka kwa Mkuu wa Wilaya Bahi


Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri wakati akipokea Mwenge wa Uhuru Mwaka 2025 kutoka kwa Mkuu wa Wilaya Bahi tukio lililofanyika katika uwanja wa Ofisi ya Afisa Mtendaji Kata ya Chigongwe jijini Dodoma.

Shekimweri alisema kuwa Mwenge wa Uhuru Mwaka 2025 ukiwa katika Wilaya ya Dodoma utachochea maendeleo. “Mimi Jabir Mussa Shekimweri, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, nakiri kuupokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Mheshimiwa Joachim Nyingo ukiwa unawaka, unang’aa na unameremeta. Aidha, nakiri kuwapokea wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa wakiwa na afya njema. Mwenge wa Uhuru ukiwa katika Wilaya ya Dodoma, utakimbizwa umbali wa kilometa 70.6, utatembelea miradi ya maendeleo saba yenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 11.1” alisema Shekimweri.

Awali akitoa taarifa fupi ya Mwenge wa Uhuru Mwaka 2025 kwa Wilaya ya Bahi, Mkuu wa Wilaya hiyo, Joachim Nyingo alisema kuwa wilaya yake ilifanikisha Mbio za Mwenge wa Uhuru salama. Alisema kuwa Mwenge wa Uhuru wilayani Bahi ulikimbizwa umbali wa kilometa 164, ulitembelea, kukagua na kuweka mawe ya msingi miradi sita yenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 1.5.



Akiongelea msisitizo wa Mwenge wa Uhuru wilayani kwake alisema kuwa ni ushiriki wa wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Msisitizo mwingine aliutaja kuwa ni matumizi ya nishati safi kwa ajili ya kutunza mazingira na uzalendo katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo