Shule ya Viziwi Dodoma yapokea msaada wa matendo ya huruma
Na. Emanuel Charles, DODOMA
Shule ya Viziwi Dodoma yakabidhiwa msaada wa mahitaji
muhimu ya kijamii yenye thamani ya shilingi 2,00,000 ikiwa ni sehemu ya matendo
ya huruma yaliyoandaliwa na Dodoma Jiji Day kwa lengo la kuhimiza upendo,
ushirikiano na mshikamano.
Msaada huo ulikabidhiwa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri katika shule hiyo iliyopo Kisasa jijini Dodoma ambapo alikabidhi mchele, sukari, vifaa vya usafi na taulo za kike.
Alisema kuwa ipo thawabu ya utoaji na kuwajali
watu wenye mahitaji maalum. “Kutoa
siyo utajiri, ni moyo. Japokuwa tulichotoa kinaweza kuonekana kidogo kwa namna
moja ama nyingine, lakini naamini kitaenda kuwasaidia watoto hawa, hasa katika
kupata chakula shuleni na kuboresha mazingira yao ya kujifunzia” alisema Alhaj Shekimweri.
Aidha,
aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa mpango wake wa kuibadilisha shule
hiyo kuwa ya mchanganyiko ili kuwaunganisha watoto wenye mahitaji maalumu ya
usikivu na wale wasio na changamoto, hatua itakayoongeza ujumuishwaji na weledi
kwa pande zote.
Kwa
upande wake, Mkuu wa Divisheni ya Maendeleo ya Jamii Jiji la Dodoma, Charity
Sichona alisema kuwa
msaada huo ni sehemu ya muendelezo wa matendo
ya huruma kufuatia sherehe ya kuuaga mwaka 2025 na
kuukaribisha mwaka 2026. “Tuliona
ni muhimu watoto hawa nao kujihisi
ni sehemu ya sherehe za jiji letu, ndiyo maana tukaandaa
bajeti ya shilingi 2,000,000 kwa ajili ya kununua mahitaji haya na kuwakumbuka”
alisema Sichona.
Nae, Mwalimu Mkuu wa Shule ya
Viziwi Dodoma, Mwl.
Awadhi Mbogo aliipongeza serikali
kwa kuendelea kuiunga mkono shule hiyo. “Tunaishukuru sana serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja
na Jiji la Dodoma, mbali na mahitaji tuliyopokea leo, tumekuwa
tukipokea shilingi 5,000,000
kila mwezi kwaajili ya kuwahudumia watoto wenye changamoto ya usikivu. Huu umekuwa
msaada mkubwa katika kuboresha lishe na mazingira yao ya kujifunzia” alisema Mwl. Mbogo.
MWISHO
Comments
Post a Comment