Jiji la Dodoma kuchangamkia fursa ujio wa Bandari Kavu Ihumwa
Na. Nancy Kivuyo, DODOMA
MSTAHIKI Meya wa Jiji la Dodoma,
Alimwoni Chaula
apongeza Mkakati wa Uendelezaji Bandari Kavu na kuahidi kujipanga kuhakikisha
wafanyabiashara wadogo wanapata fursa ya kufanya biashara katika eneo hilo na
kuchochea ukuaji wa uchumi wa mkoa na taifa kwa ujumla.
Akizungumza katika ziara
ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwenye Bandari Kavu Ihumwa iliyokuwa na lengo la
kujiridhisha na mkakati wa uendelezaji wa miundombinu hiyo, alisema kuwa uongozi
wa jiji utakaa kikao na kutathmini namna ya kuandaa mazingira rafiki ya
biashara ili kuwawezesha wajasiriamali wa ndani kushiriki kikamilifu katika
shughuli za upokeaji, uhifadhi na usafirishaji wa mizigo.
Alieleza kuwa pamoja na
fursa za moja kwa moja zitakazotokana na shughuli za bandari hiyo, jiji pia
linatarajia kuimarisha sekta ya usafirishaji, uhudumu na biashara ndogondogo
hivyo kuongeza ajira na kipato kwa wananchi.
Aidha, Mstahiki Meya
Chaula aliongeza kuwa jiji litafanya utaratibu wa kufanya mazungumzo na Mamlaka
ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) ili kuweka utaratibu mzuri wa
usafiri wa kufika katika Bandari Kavu na kurejea katikati ya jiji. Alisisitiza
kuwa mpango huo utasaidia kupunguza changamoto za usafiri kwa wafanyabiashara
na wananchi pamoja na kurahisisha mzunguko wa bidhaa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi
wa Ardhi na Majengo kutoka Shirika la Reli Tanzania (TRC), Kokwika Ishenkumba alieleza
kuwa wapo kwenye mazungumzo na Jiji la Dodoma ya kupata hati ya eneo hilo ili
kurasimisha ardhi na kuweza kuitumia kikamilifu kama ambavyo wamekusidia ili
kuleta tija kiuchumi. “Tupo kwenye mazungumzo na Jiji la Dodoma, tuna imani
kuwa tutafanikiwa kupata hati ili tuweze kutumia eneo letu sasa kikamilifu
kufanya miradi ambayo tumeazimia tukizingatia ushauri wa Mheshimiwa Mkuu wa
Mkoa wa Dodoma kuelekea ujio wa AFCON mwaka 2027” alisema Ishenkumba.
MWISHO
Comments
Post a Comment