Elimu ya utunzaji zao la Zabibu yawafikia wananchi Jiji la Dodoma
Na. Veronica, NANENANE DODOMA
Afisa
Kilimo Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Emanuel Mayyo ametoa elimu juu ya
utunzaji wa kilimo cha zabibu kuanzia upandaji hadi uvunaji ili kiwe na tija
kwa wakulima.
Hayo aliyasema katika viwanja vya maonesho ya Nanenane wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea vipando bustani vya Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Alisema kuwa kuna umuhimu wa kulima zao la zabibu kwasababu ni zao lenye faida katika sekta ya biashara na kuwakwamua kiuchumi wananchi wa Jiji la Dodoma. “Zao la zabibu ni zao mama hapa Dodoma na ni zao ambalo linafaida kubwa kwa wakulima. Hivyo, kuna haja ya wale wakulima ambao wanahitaji kulima zao hili kujifunza na kutambua hatua zote za zao hili kuanzia upandaji hadi uvunaji ili kupata zao bora,” alisema Mayyo.
Pia aliongeza kusema kuwa kuna mpango wa kuweka mkataba na baadhi ya makampuni ili wananchi wa Jiji la Dodoma waweze kupata soko la zao hilo. “Vilevile, tuna mpango madhubuti kwa wale wakulima wanao lima zao hili kwa kuingia mkataba na makampuni ambayo yanazalisha mvinyo ili wakulima waweze kuuza mazao yao na kupata soko la uhakika ili kujikwamua kiuchumi,” alisema Mayyo.
Kwa upande wake mkulima wa zao hilo za zabibu, Sadiki Nasoro aliwashukuru maafisa hao kwa kuwapatia elimu hiyo na kuahidi kuwa watafanyia kazi yote waliyojifunza. Mwitikio wa msimu huu umekuwa mkubwa sana tofauti na msimu uliopita maandalizi ni mazuri kwasababu maboresho ya sekta ya utoaji elimu yamenifurahisha nimeweza kupata elimu bora kuhusiana na zao la zabibu jinsi ya kuzalisha miche. Sikutegemea kama nitenda maonesho ya Nanenane kupata elimu ya kipando cha zao la zabibu ni kitu ambacho kimenishangaza na nitakuwa balozi mzuri wa kuwahamasisha wakulima wengine jinsi ya kufika na kupata elimu bora,’’ alisema Nasoro.
MWISHO
Imehaririwa na Tutindaga Nkwindi
Comments
Post a Comment