Kata ya Kizota yajivunia maendeleo makubwa ya miradi
Na. Asteria Frank, DODOMA
Diwani wa Kata ya Kizota, Jamal Ngallya
afurahia mafanikio ya serikali kwa kipindi cha miaka minne ya utekelezaji wa
miradi ya maendeleo ya Kituo cha Afya, Shule ya Msingi Mahungu na stendi ya
mabasi katika kata yake.
Aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kata hiyo kujionea miradi iliyotekelezwa na serikali katika Kata ya Kizota.
Alisema kuwa katika kipindi cha miaka
minne ya serikali ya awamu ya sita, kata hiyo imeshuhudia maendeleo makubwa. “Mimi
leo naweza kuzungumza kuwa Kizota ya sasa hivi na ya miaka 10 nyuma ni vitu
viwili tofauti, wakati mimi nazaliwa tulikuwa tunapata huduma za afya Makole na
taasisi ya Magereza Isanga lakini leo Kizota tunatamba tumepata kituo cha afya
kikubwa ambacho kinagharimu kiasi cha zaidi ya shilingi 500,000,000 ambapo kwa
Dodoma sasa hivi kituo hicho kitashika nafasi ya tatu kwa ukubwa na hivi karibuni
kitaenda kufunguliwa ili kitoe huduma mbalimbali kwa wananchi” alisema Ngallya.
Aliongeza kuwa serikali imetoa fedha
kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya mabasi ambayo itahudumia wananchi wengi.
“Ila pia mama ametoa bilioni sita
kwaajili ya ujenzi wa stendi ya kisasa ambayo itakuwa stedi ya pili kwa ukubwa
baada ya stendi ya Nanenane. Stendi hiyo pia itahudumia magari yanayotoka
ukanda wa magharibi kama Kigoma, Musoma na Tabora. Stendi hiyo itakuwa na uwezo
wa kubeba mabasi zaidi ya 200 na mkandarasi alishasaini mkataba wa ujenzi wa
stendi hiyo” aliongeza Ngallya.
Nae Afisa Mtendaji wa Kata ya Kizota, Aidan
Libenanga alisema kuwa suala la utawala bora linafanyika kwa uthabiti. Migogoro
ya ardhi imepungua sana kutokana na mkakati wa kuitatua kufanikiwa.
Akiongelea suala la lishe, alisema kuwa kata imekuwa ikiadhimisha maadhimisho ya siku ya afya na lishe kila baada ya robo mwaka kwa mitaa yote. “Kwa upande wa lishe bora huwa tunaadhimisha kwa ngazi za mitaa kila baada ya robo mwaka kwa kuwashirikisha jamii inayotuzunguka kwa kuwapa elimu ya lishe. Tumekuwa tukiwashirikisha wataalam wa afya kutoka maeneo mbalimbali kwa ajili ya kutoa elimu kwa vitendo ili wananchi waweze kuona na kuelewa kwa urahisi” alisema Libenanga.
Katika hatua nyingine Mkazi wa Mtaa wa Mbuyuni, Kata ya Kizota, Steven Kapangala alishukuru mafanikio ya serikali ya awamu ya sita kwa kuwapelekea miradi mikubwa ya maendeleo kama stendi ya mabasi kwa sababu itasaidia kufungua fursa za kiuchumi kwa wafanyabiashara na wajasiriamali. “Lengo kubwa la serikali ni kutusaidia zaidi kuboresha mazingira ya kufanya biashara katika mazingira rafiki yenye kufikika na yenye tija lakini mradi huu wa wa stendi utatuletea maendeleo makubwa sana hasa katika mkoa wetu wa Dodoma” alisema Kapangala.
Kwa upande mwingine mkazi wa Kata ya Kizota, Rachel John, aliishukuru serikali kwa kusikia kilio chao cha kutaka stendi ya Kizota iboreshwe. “Mradi utakapoanza tutakuwa na fursa ya kufanya biashara na tutapata maendeleo kwa hakika tutafanya mambo mazuri. Mimi kama mama lishe naamini nitaweza kufanya sana biashara” alisema John.
MWISHO
Comments
Post a Comment