Ujenzi Queens bega kwa bega na Mwenge wa Uhuru, 2026 Dodoma


Na. Dennis Gondwe, DODOMA

WIZARA ya Ujenzi inaunga mkono Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 utakaoanza mbio zake tarehe 1 Juni, 2026 katika Wilaya ya Dodoma kwa kushiriki katika mashindano ya Mwenge Super Cup yakilenga kuhamasisha jamii kujiandaa na mapokezi ya Mwenge huo kwa kudumisha amani na umoja wa kitaifa.


Kocha wa Timu ya Wizara ya Ujenzi (Ujenzi Queens), Mwamvita Mzee

Kauli hiyo ilitolewa na Kocha wa Mchezo wa Mpira wa Pete wa Timu ya Wizara ya Ujenzi (Ujenzi Queens), Mwamvita Mzee alipokuwa akiongea na mwandishi wetu muda mfupi kabla ya kuanza mchezo wao na Timu ya Mpira wa Pete ya Dodoma Jiji katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.


Mzee alisema kuwa hamasa ya Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 kwa wanamichezo ni kubwa katika Wilaya ya Dodoma. “Sisi Timu ya Mpira wa Pete ya Wizara ya Ujenzi tumehamasika kuja kuunga mkono ujio wa Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 katika Wilaya ya Dodoma. Lengo ni kuonesha umoja na mshikamano baina ya wanamichezo kama dhamira ya Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 ilivyo ya kuleta umoja na mshikamano wa kitaifa” alisema Mzee.


Kwa upande wake Afisa Michezo Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Neema Kilongola alisema kuwa mashindano ya Mwenge Super Cup yanalenga kuwahamasisha wanamichezo na wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye mapokezi ya Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 katika Wilaya ya Dodoma. Hamasa hiyo ni pamoja na kujitokeza kwa wingi katika maeneo yote yatakayopitiwa na Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026.


Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 unaongozwa na kaulimbiu isemayo “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo”.






MWISHO  

 

Comments

Popular Posts

Dodoma Jiji yaangukia pua dhidi ya Ujenzi Queens Mwenge Super Cup

Afisa Elimu Jiji la Dodoma anunua jina la Rais Samia kwa Laki 5