Dodoma Jiji yaangukia pua dhidi ya Ujenzi Queens Mwenge Super Cup
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
TIMU ya Mpira wa Pete ya Wizara ya Ujenzi (Ujenzi
Queens) imeibuka kidedea kwa kuifunga Timu ya Mpira wa Pete ya Dodoma Jiji kwa
magoli 37-33 katika mchezo wa kuvutia uliochezwa katika viwanja vya Chinangali
Park.
Mchezo huo ulianza kwa kasi ya kawaida na kuendelea kushika kasi kadri muda ulivyokuwa ukisogea.
Hadi mchezo unamalizika, Timu ya Ujenzi Queens
iliikuba na ushindi wa magoli 37 dhidi ya 33 ya Dodoma Jiji.
Awali Kocha wa Timu ya Mpira wa Pete ya Ujenzi Queens
Mwamvita Mzee alisema kuwa wamekuwa wakipata matokeo mazuri kutokana na kufanya
mazoezi mara kwa mara. “Timu yetu inaamini katika mazoezi ya mara kwa mara. Kama
unavyofahamu mazoezi hayadanganyi, tumekuwa tukifanya mazoezi kwa bidii ndiyo
siri ya mafanikio yetu. Zidi ni kupendana kama timu na watu kujitoa kwa ajili
ya timu na kuupenda mchezo. Pia, kwetu ni utekelezaji wa maelekezo ya
Mheshimiwa Rais wa Tanzania ya kufanya mazoezi kwa watumishi mahala pa kazi”
alisema Mzee.
Kwa upande wake Afisa Michezo Halmashauri ya Jiji la
Dodoma, Neema Kilongola alisema kuwa mashindano ya Mwenge Super Cup Mwaka 2026 yanalenga
kuwahamasisha wanamichezo na wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye mapokezi ya
Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 katika Wilaya ya Dodoma.
MWISHO
Comments
Post a Comment