TANESCO Ddodoma kuendelea kuboresha miundombinu ya umeme Jiji la Dodoma

Na. Mwandishi Wetu-DODOMA

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Dodoma limetoa semina kwa madiwani wa kata zote 41 za Jiji la Dodoma lengo likiwa ni kueleza mikakati ya shirika hilo pamoja na miradi inayotekelezwa katika Mkoa wa Dodoma.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Dodoma, Charles Mamba,akizungumza wakati akifungua Mkutano wa Madiwani, kamati ya ulinzi na Usalama Wilaya na Polisi kata wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ulioandaliwa na Shirika la Umeme (TANESCO) Mkoa wa Dodoma


Akitoa elimu jijini Dodoma, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Mhandisi Donasiano Shamba alisema kikao hicho kimejumuisha Madiwani, Kamati ya Usalama Wilaya na Polisi kata wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

“Kikao hiki kimehusisha madiwani kutoka kata zote 41 za Jiji la Dodoma pamoja na Polisi kata lengo ni kueleza mikakati yetu lakini pia kueleza changamoto zinazotukabili sisi kama shirika hasa suala la uharibifu wa miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme” alisema Mhandisi Shamba.

Aidha, alisema kwa kuwashirikisha madiwani hao kwenye kikao hicho watakuwa wamewafikia watu zaidi ya 700,000 wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Dodoma hakuna uhaba wa umeme bali shida iliyopo ni ubovu wa miundombinu ambayo inachangia kukatika kwa umeme mara kwa mara, aliongeza.

Alielezea kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/24 Shirika la Umeme Tanzania Mkoa wa Dodoma, limetengewa kiasi cha Shilingi bilioni 14, kwa ajili ya kupeleka nishati hiyo kwa wananchi na kukarabati miundombinu ili kumaliza tatizo la kukatika kwa umeme.

“Katika mwaka huu wa fedha tumepatiwa kiasi cha shilingi bilioni 14 na kati ya hizo bilioni sita ni kwa ajili ya kuboresha miundombinu yetu na kiasi kingine ni kwa ajili ya kupeleka umeme maeneo ya karibu na wananchi” alisema Mhandisi Shamba.

Awali Afisa Usalama wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Madega Dudu, alisema shida inayowakabili hivi sasa ni pamoja na uharibifu wa miundombinu ya kusafirishia na kusambazia umeme. "Hivi sasa kumekuwepo na shida ya wizi wa vyuma kwenye miundombinu ya kusafirishia (Grid) umeme, mafuta ya transfoma, nyaya za kopa pamoja na miundombinu ya usalama kwenye mashine umba (Transfoma). Tunaomba wananchi kutoa taarifa dhidi ya watu hawa ambao wanajihusisha na uharibifu wa miundombinu hii, tafiti zinaonyesha mafuta ya transfoma wanayoiba kwa kiasi yanachanganywa na mafuta ya kukaangia chipsi lakini pia mikoa ya kanda ya ziwa na bahari yanatumika kukaangia samaki. Na wengine wanayatumia kwa ajili ya vipodozi na kiasi kikubwa yanatumika kutengenezea vilainishi vya mitambo” alisema Dudu.

Afisa Usalama wa TANESCO mkoa wa Dodoma, Madega Dudu akitoa elimu kuhusu uharibifu wa miundombinu ya kusafirishia na kusambazia umeme wakati wa Mkutano wa Madiwani, kamati ya Usalama Wilaya na Polisi kata wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma 


Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe alilipongeza shirika hilo Mkoa wa Dodoma kwa kuboresha huduma ya nishati katika mkoa huo na kuendelea kuwafikia wateja kwa wakati pindi inapotokea changamoto yoyote.

Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma Prof. Davis Mwamfupe akizungumza wakati wa Mkutano wa Madiwani, kamati ya Usalama Wilaya na Polisi kata wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ulioandaliwa na Shirika la Umeme (TANESCO) Mkoa wa Dodoma


"Sisi kama Madiwani tunawapongeza TANESCO Mkoa wa Dodoma kwa kuendelea kutoa huduma bora ya nishati Mkoa wa Dodoma hakuna changamoto kubwa ya umeme hata inapotokea mnatatua kwa wakati na kuwafikia wateja wenu kwa wakati kwa hilo tunawapongeza sana" alisema Prof. Mwamfupe.

Nae Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Dodoma Charles Mamba aliyekuwa mgeni rasmi akifunga semina hiyo aliwataka madiwani kwenda kuwa mabalozi wazuri katika kusimamia miundombimu ya umeme kwa kutoa elimu kwa wananchi wa maeneo yao.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Dodoma, Charles Mamba,akizungumza wakati akifungua Mkutano wa Madiwani, kamati ya ulinzi na Usalama Wilaya na Polisi kata wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ulioandaliwa na Shirika la Umeme (TANESCO) Mkoa wa Dodoma


"Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, DKt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwajali wananchi wake kwa kuwaletea huduma bora za nishati na kwa mikakati ya TANESCO hapa Makao Makuu ya nchi, shida ya umeme inaenda kuwa historia" alisema Mamba.

 





Chanzo Blog ya Michuzi

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma