Kata ya Chamwino yatakiwa kuchukua tahadhari ya Kipindupindu
Na. Dennis Gondwe, CHAMWINO
HALMASHAURI
ya Jiji la Dodoma imefurahishwa na muitikio wa wakazi wa Kata ya Chamwino
kushiriki katika mazoezi ya usafi wa mazingira na kuwataka kuendelea kuchukua
tahadhari dhidi ya ugonjwa wa kipindupindu.
![]() |
Mkuu wa Kitengo cha Usafi na udhibiti taka ngumu wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro akiongea na mamia ya wakazi wa Kata ya Chamwino |
Kauli
hiyo ilitolewa na Mkuu wa Kitengo cha Usafi na udhibiti taka ngumu wa Halmashauri
ya Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro alipokuwa akiongea na mamia ya wakazi wa Kata
ya Chamwino waliojitokeza kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo.
Kimaro
alisema “nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wakazi wa Kata ya Chamwino kwa
jinsi mlivyojitokeza kwa wingi kufanya usafi katika eneo la makaburi ya Hijra
na maeneo mengine ya kata. Tulichokifanya hapa ni ibada tosha kwa sababu
tumesafisha eneo tulipowalaza ndugu zetu. Lakini niwapongeze kwasababu mmekuwa
mkijitokeza kwa wingi kufanya usafi katika makazi na maeneo yanayowazunguka”.
![]() |
Wakazi wa Chamwino wakishiriki zoezi la usafi |
Akiongelea
tahadhari ya ugonjwa wa kipindupindu aliwataka wakazi hao kuendelea kuchukua
tahadhari. “Ndugu zangu, tuendelee kufanya usafi kwenye makazi yetu, amesema
hapa mwenyekiti wetu kuwa tunatoa tahadhari kwa ajili ya ugonjwa wa
kipindupindu. Na tumaini mmesikia kwenye vyombo vya habari kuwa ugonjwa wa
kipindupindu upo katika baadhi ya maeneo nchini. Serikali imeshaanza kutoa
tahadhari na halmashauri tunaendelea kusisitiza juu ya tahadhari hiyo. Ndugu
zangu uwepo wa kipindupindu unatokana na uchafu na hasa kula kinyesi. Maana
yake kuna sehemu usafi haukufanyika vizuri ukaacha nzi wakaingia kwenye vyakula
na sisi tukala tukapata kipindupindu. Hivyo, jinsi ya kujikinga ni kufanya
usafi kwenye makazi yetu” alisisitiza Kimaro.
Kwa
upande wake Mkazi wa Kata ya Chamwino, Mwanaidi Juma alisema kuwa Halmashauri
ya Jiji imejitahidi kutoa elimu juu ya usafi wa mazingira. “Niseme ukweli,
suala la usafi na umuhimu wake tumeelezwa sana na halmashauri. Ni jukumu letu
kufanya usafi wa mazingira. Natamani ifike wakati suala la usafi wa mazingira
liwe ni utamaduni wetu na siyo kusubiri serikali kutuhamasisha kufanya usafi.
Mfano bwana Kimaro kaongelea suala la kipindupindi, mtu akipata kipindupindu,
inayoathirika ya kwanza ni familia yake na mtu akifa hawezi kurudi. Maana yake
ni bora kuchukua tahadhari ya usafi ili tuendelee kuwa salama” alisema
Juma.
Usafi
wa pamoja siku ya Jumamisi umefanyika katika Kata ya Chamwino ukihusisha
maafisa waandamizi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, mamia ya wakazi wa kata
hiyo na Mbunge wa Jimbo la Urambo alikuwa sehemu ya washiriki.
Mbunge wa Urambo Mhe Magreth Sitta (kushoto) akifurahia jambo na Mkuu wa Kitengo cha Usafi na uthibiti wa taka ngumu Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro baada ya kushiriki zoezi la usafi wa mazingira |
MWISHO
Comments
Post a Comment