Makala: Tanzania inavyojiandaa kuvuna matunda ya AFCON 2027
Na. John Walter, Manyara
Mwezi Juni mwaka
2027 utaingia kwenye historia ya Tanzania kwa maandishi yasiyofutika kirahisi.
Kwa mara ya kwanza tangu kupata uhuru, Tanzania itakuwa mwenyeji wa mashindano makubwa zaidi ya soka barani Afrika, Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), yatakayoandaliwa kwa ushirikiano wa nchi tatu za Afrika Mashariki; Tanzania, Kenya na Uganda.
Kwa wengi, AFCON ni
mashindano ya mpira wa miguu yanayodumu kwa siku 30 pekee.
Lakini kwa wachumi,
wawekezaji na wafanyabiashara wadogo, ni injini kubwa ya uchumi inayoweza
kuingiza mabilioni ya fedha, kuzalisha ajira na kuitangaza Tanzania mbele ya
mamilioni ya watu duniani.
Tayari maandalizi
yameanza kuonekana kupitia miradi mikubwa ya miundombinu inayotekelezwa katika
maeneo mbalimbali nchini.
Mkoa wa Arusha,
ambao umetajwa kuwa miongoni mwa wenyeji wa mashindano hayo, unashuhudia ujenzi
wa Uwanja wa Kisasa wa Samia Suluhu Hassan katika eneo la Olmot.
Uwanja huo wenye
uwezo wa kubeba mashabiki 30,000 umefikia zaidi ya asilimia 83 ya ujenzi na
unatarajiwa kukamilika mwezi Agosti 2026.
Uwekezaji huo wa
miundombinu tayari umeanza kuvutia pongezi kutoka kwa wadau wa soka duniani.
Mwezi Mei 2026,
nyota wa zamani wa timu ya taifa ya Uingereza na klabu ya Manchester United,
Rio Ferdinand, alipotembelea Uwanja wa Samia Suluhu Hassan unaojengwa Arusha,
aliusifu kwa kuzingatia viwango vya kisasa vya kimataifa.
“Nimecheza kwenye viwanja vingi duniani lakini kiwanja hiki ni kizuri na chenye viwango. Niwapongeze wajenzi, wakandarasi na wataalamu wote wanaofanya kazi hii nzuri,” alinukuliwa akisema wakati wa ziara yake nchini.
Hata hivyo, nyuma
ya zege, nondo na vifaa vya kisasa vinavyojenga uwanja huo, kuna ndoto na
matumaini ya maelfu ya wananchi wanaotarajia kunufaika na AFCON.
Mubaraka Sungi,
mkazi wa Arusha, anaamini mashindano hayo yatafungua milango ya fursa kwa
wananchi wa kawaida.
“Wenye hoteli
watanufaika, mama ntilie watanufaika, boda boda watanufaika, hata wauza bidhaa
za asili watanufaika. Kutakuwa na fedha nyingi zinazozunguka kwa muda mfupi,”
anasema.
Kwa mtazamo wake,
AFCON si tukio la michezo pekee bali ni uchumi unaotembea kutoka kwa mgeni
mmoja kwenda kwa mamia ya wananchi wanaotoa huduma mbalimbali.
Mtazamo huo
unaungwa mkono na Alex Mlai ambaye anaona manufaa ya mashindano hayo yatafika
hata katika mikoa inayozunguka Arusha.
“Babati nayo
itanufaika. Wageni wengine watatafuta malazi nje ya Arusha, wengine watanunua
huduma mbalimbali njiani. Huu ni uchumi wa watu wa kawaida,” anasema.
Katika pembezoni
mwa barabara kuu ya Arusha–Babati, Jenipha Alphonce amekuwa akitengeneza na
kuuza bidhaa za asili ikiwemo vikapu, mikeka, shuka za Kimasai, kofia na
mapambo mbalimbali yanayovutia watalii.
Anasema ukuaji wa
sekta ya utalii umeongeza wateja kutoka mataifa mbalimbali tofauti na zamani
walipokuwa wakitegemea zaidi wateja wa ndani.
“Sasa tunapokea
wageni wengi kutoka nje ya nchi. Kuelekea AFCON 2027 tunajipanga kuongeza
uzalishaji wa bidhaa na kuboresha ubunifu ili wageni watakaokuja wapate huduma
bora,” anasema.
Jenipha anaamini
bidhaa za asili za Tanzania zitakuwa mabalozi wa kuitangaza nchi kimataifa kwa
sababu zinawakilisha utamaduni na urithi wa Watanzania huku zikiwa rafiki kwa mazingira.
Kwa mujibu wa
makadirio ya Serikali, Tanzania inatarajia kupokea wastani wa mashabiki na
watalii takribani 300,000 kwa siku katika kipindi cha mashindano hayo.
Iwapo maandalizi
yatafanyika kwa ufanisi, idadi hiyo inaweza kuongeza kwa kiwango kikubwa
matumizi katika sekta za hoteli, usafirishaji, chakula, biashara za fedha,
utalii, burudani na mawasiliano.
Uzoefu wa mataifa
mengine unaonyesha namna mashindano ya AFCON yanavyoweza kubadilisha uchumi wa
nchi mwenyeji.
Morocco, ambayo
iliandaa michuano mikubwa ya Afrika kwa mafanikio makubwa, ilivunja rekodi ya
watazamaji kwa kuvutia mashabiki zaidi ya 729,000 katika hatua ya makundi
pekee. Nchi hiyo ilikadiriwa kupokea kati ya mashabiki 600,000 hadi milioni
moja kutoka mataifa mbalimbali na kuingiza zaidi ya Euro bilioni moja kupitia
shughuli zilizohusiana na mashindano hayo.
Mchambuzi wa
masuala ya uchumi na siasa, Hamduni Marcel, anaeleza kuwa mafanikio ya kiuchumi
ya AFCON yatategemea uwezo wa Tanzania kutumia vizuri fursa zinazokuja pamoja
na mashindano hayo.
Anasema sekta ya
utalii, hoteli, usafiri, biashara za kubadilisha fedha na huduma nyingine
zitakuwa miongoni mwa wanufaika wakubwa.
“Jambo hili halina
mashaka kuhusu uchumi kukua. Arusha ni jiji la wachacharikaji. Kinachohitajika
sasa ni maandalizi ya pamoja ya taasisi zote husika ili kuhakikisha wananchi
wengi zaidi wanajua fursa zilizopo na wanajiandaa kuzitumia,” anasema.
Anashauri Bodi ya
Utalii Tanzania, Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja
na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kushirikiana kwa karibu katika
kuitangaza AFCON mapema ili kuvutia wageni wengi zaidi.
Mbali na mapato ya
moja kwa moja, AFCON inaacha urithi wa muda mrefu kupitia miundombinu.
Barabara
zinazojengwa leo zitatumika hata baada ya mashindano kuisha. Viwanja vya ndege
vitabaki kuhudumia wasafiri.
Hoteli zitabaki
kupokea wageni. Viwanja vya michezo vitatumika kuibua vipaji vya vijana wa
Tanzania kwa miaka mingi ijayo.
Dar es Salaam
kupitia Uwanja wa Benjamin Mkapa, Zanzibar kupitia Uwanja wa Fumba na Arusha
kupitia Uwanja wa Samia Suluhu Hassan vitakuwa vituo muhimu vya mashindano
hayo.
Waziri wa Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema Serikali imejipanga kuifanya
Arusha kuwa kitovu cha michezo nchini kupitia uwekezaji mkubwa katika
miundombinu na programu za kuendeleza vipaji vya vijana.
Hii inaonyesha kuwa
AFCON si tukio la mwezi mmoja pekee, bali ni sehemu ya mkakati mpana wa kukuza
michezo, utalii na uchumi wa taifa.
Aidha, Arusha ikiwa
lango la utalii nchini, wageni watakaokuja kushuhudia AFCON watapata nafasi ya
kutembelea Hifadhi ya Serengeti, Tarangire,Arusha national Park, Eneo la
Hifadhi la Ngorongoro na Mlima Kilimanjaro.
Hivyo, mashindano
hayo yatakuwa maonesho makubwa ya vivutio vya Tanzania mbele ya dunia.
Kwa wafanyabiashara
wadogo, huu ni wakati wa kuuza bidhaa, huduma na utamaduni wa Tanzania.
Kwa vijana
wanaotafuta ajira, ni fursa ya kupata kipato kupitia sekta mbalimbali
zitakazohitaji nguvu kazi ya muda na ya kudumu.
Kwa mara ya kwanza
katika historia ya Afrika Mashariki, nchi tatu zimeungana kuandaa mashindano
makubwa kiasi hiki. Ushirikiano huo unaimarisha diplomasia ya uchumi, biashara
na mahusiano ya kikanda.
AFCON 2027 si
mashindano ya soka pekee. Ni mtihani wa uwezo wa Tanzania kutumia michezo kama
chachu ya maendeleo. Wakati mashabiki watakapokuwa wakishangilia magoli
viwanjani, maelfu ya Watanzania watakuwa wakivuna matunda ya ajira, biashara na
utalii.
Na filimbi ya
mwisho itakapopulizwa Julai 2027, ushindi mkubwa zaidi huenda usiwe wa nchi
itakayochukua kombe, bali w
a Tanzania
itakayokuwa imejijengea uchumi, hadhi na fursa mpya mbele ya dunia.
Comments
Post a Comment