CCM yaridhishwa na miradi Jiji la Dodoma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Dodoma kimeridhishwa na utendaji kazi wa serikali baada ya kutembelea na kukagua miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya shilingi 600,424,100,099 inayotekelezwa katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

 

Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa, Donald Mejiti akiongea wakati wa majumuisho ya ziara ya Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Dodoma

Kauli hiyo ilitolewa na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa, Donald Mejiti alipoongoza Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Dodoma kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

 

Mejiti alisema kuwa kazi iliyofanyika ni kubwa na nzuri. Alisema kuwa timu yake imetembelea na kukagua miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya shilingi 600,424,100,099 na kujiridhisha kuwa imetekelezwa kwa kiwango bora.

 

Aidha, alipongeza ushirikiano baina ya serikali na Chama Cha Mapinduzi kuwa ni mzuri. “Ndugu zangu tunapopita katika ziara zetu, pia tunaangalia uhusiano baina ya serikali na chama. Hapa Halmashauri ya Jiji la Dodoma uhusiano huo ni mzuri na ndiyo siri ya mafanikio. CCM hakuna sehemu tumeona tunakwamishwa na serikali. Kila mradi tulioukagua umejengwa vizuri na unavutia” alisema Mejiti.

 

Wakati huohuo, aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kupunguza migogoro ya Ardhi. Alisema kuwa ushirikiano baina ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma umewezesha kupunguza migogoro ya Ardhi. “Miongoni mwa ushahidi ni kwamba malalamiko yanayokuja Ofisi ya CCM Mkoa wa Dodoma yamepungua sana. Ushahidi mwingine ni juhudi za Halmashauri ya Jiji la Dodoma kulipa fidia wananchi waliokuwa wakidai” alisema Mejiti.

 CCM 


Katika hatua nyingine Mbunge wa Jimbo la Dodoma mjini, Anthony Mavunde aliahidi kuchangia shilingi milioni 15 ujenzi wa nyumba ya Mkuu wa Shule ya Sekondari Zuzu na shilingi milioni tano ununuzi wa viti na meza kwa Shule ya Msingi Iyumbu.

 

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri akitoa neno la utangulizi

Awali akimkaribisha Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi Taifa, katika Wilaya ya Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabi Shekimweri alimtaarifu kuwa timu yake ipo timamu katika kutekeleza miradi ya maendeleo na miradi yote ipo sawasawa. “Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan namna anavyotoa fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Dodoma. Leo utatembelea miradi saba yenye thamani ya shilingi bilioni 600,424,100,099” alisema Alhaj Shekimweri.

 

Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Dodoma ilitembelea mradi wa ujenzi wa vyumba nane vya madarasa na matundu 10 ya vyoo Shule ya Sekondari Zuzu, ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Dodoma, mradi wa ujenzi wa Barabara ya Mzunguko wa Nje, ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa Msalato, ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo, mradi wa Maji Nzuguni na ukarabati wa vyumba 10 vya madarasa Shule ya Msingi Iyumbu.

 
MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma