RC Senyamule aagiza utengenezaji Viti uende sambamba na ujenzi wa madarasa Sekondari Mtumba

Na. Dennis Gondwe, MTUMBA

MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule ameagiza ujenzi wa madarasa uende sambamba ya utengenezaji wa viti na meza kwa ajili ya wanafunzi ili vyote vikamilike pamoja na kuanza kutoa huduma.


Kauli hiyo aliitoa alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa madarasa nane na matundu 10 ya vyoo katika Shule ya Sekondari Mtumba iliyopo Kata ya Mtumba, Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Baada ya kukagua hatua ya ujenzi wa miundombinu hiyo alihoji hatua ya utengenezaji wa viti na meza ambao ulikuwa haujaanza. Mkuu wa Mkoa wa Dodoma aliagiza utaratibu wa kutengeneza viti na meza uanze ili uende sambamba ya ujenzi wa miundombinu hiyo na kukamilika pamoja ili isicheleweshe utoaji wa huduma.

Akisoma taarifa ya ujenzi wa madarasa nane na matundu 10 ya vyoo kwa ajili ya mapokezi ya wanafunzi wa kidato cha tano mwaka 2024/2025 Mkuu wa Shule ya Sekondari Mtumba, Mwl. Stephen Moshi alisema kuwa ujenzi unaendelea vizuri. “Shule ilipokea shilingi 201,000,000 tarehe 6 Januari, 2024 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa nane na matundu 10 ya vyoo. Kwa upande wa vyumba nane vya madarasa umekamilika kwa asilimia 100 na ujenzi wa matundu ya vyoo upo hatua ya umaliziaji sawa na asilimia 75” alisema Mwl. Moshi.

Akiongelea faida za mradi huo alizitaja kuwa ni kuwawezesha wanafunzi wa kidato cha tano kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania kupata elimu hiyo kutokana na kujengewa miundombinu wezeshi ya kufundishia na kujifunzia. Faida nyingine ni ajira wa wananchi wanaozunguka shule hiyo kutokana na shughuli mbalimbali zitakazokuwa zinafanyika.

Shule ya Sekondari Mtumba ipo katika Kata ya Mtumba umbali wa kilometa 23 kutoka katikati ya Jiji la Dodoma ikihudumia wanafunzi 641 wakidato cha kwanza hadi cha nne kutoka mitaa ya Majengo, Mtumba na Vikonje na baadhi ya wanafunzi kutoka Mahoma Makulu na Ipala.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma