RC Dodoma afurahishwa ujenzi Sekondari Mtemi Chiloloma

Na. Dennis Gondwe, HOMBOLO MAKULU

MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule ameagiza ujenzi wa Shule ya Sekondari Mtemi Chiloloma kusimamiwa vizuri ili ukamilike katika muda uliopangwa kwa ajili ya kutoa huduma.


Agizo hilo alilitoa alipofanya ziara ya kutembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa shule hiyo iliyopo katika Kata ya Hombolo Makulu, jijini Dodoma.

Awali akikagua ujenzi huo alieleza kufurahishwa kwake na hatua ya ujenzi wa shule hiyo. Aliwataka viongozi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kusimamia vizuri mradi huo ili uweze kukamilika katika muda uliopangwa.

Akisoma taarifa ya ujenzi wa vyumba nane vya madarasa na matundu 18 ya vyoo kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mkuu wa Shule ya Sekondari Mtemi Chiloloma, Mwl. Livinus Tanganyika alisema shule yake ilipokea shilingi 216,000,000 kutoka serikali kuu. “Ujenzi ulianza tarehe 25 Novemba, 2023 mpaka sasa ujenzi wa madarasa umekamilika kwa asilimia 100, matundu ya vyoo 18 yapo hatua ya umaliziaji, kazi inayoendelea ni kuweka marumaru. Mradi unategemea kukamilika kabla au ifikapo tarehe 10 Mei, 2024” alisema Mwl. Tanganyika.

Akiongelea faida za mradi huo, alisema kuwa utakapokamilika utaongeza ufaulu wa wanafunzi kwa sababu mazingira ya kufundishia na kujifunzia yatakuwa yameboreshwa. Faida nyingine aliitaja kuwa mradi unatoa ajira kwa wananchi wanaozunguka eneo hilo kuanzia kwa mafundi na wasaidizi wao.

Kwa upande wa mwananchi mkazi wa Hombolo, Jeremiah Samwel alisema kuwa kitendo cha serikali kujenga shule hiyo mpya kinaonesha dhamira ya serikali katika kujali elimu ya wananchi wake. Shule hii inawasaidia sana wananchi wa maeneo haya kwa sababu isingejengwa wanafunzi wangekosa fursa ya elimu, aliongeza.

Shule ya Sekondari Mtemi Chiloloma ipo umbali wa kilometa 54 kutoka katikati ya Jiji la Dodoma ikihudumia wanafunzi kutoka mitaa ya Zapisa, Msisi, Mayeto, Tandahima na Masea ikiwa na idadi ya wanafunzi wa kidato cha hadi cha nne 527 na walimu 10.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma