Shilingi Milioni 473 kutekeleza Mradi wa Ufungaji CCTV Kamera Jiji la Dodoma

Na. Josephina Kayugwa, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imesani mkataba na Kampuni ya Wisjane Smart Systems kwaajili ya ufungaji wa kamera za usalama barabarani (CCTV) unaogharimu shilingi 473,000,000 ikiwa ni mradi utakaotekelezwa kwa kipindi cha miezi mitatu.




Akitoa taarifa ya mradi, Mkuu wa Kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Joseph Fungo alisema kuwa mradi huo utakwenda kuimarisha ulinzi na usalama katika Jiji la Dodoma kwasababu kamera hizo zitafanya kazi masaa 24. “Mradi huu wa gharama ya shilingi 473,000,000 utahusisha ufungaji wa kamera kwenye barabara zinazoinga njia kuu lakini pia hapo baadae utakuja kuimarishwa zaidi kwa kuongeza sehemu nyingine za kuweka kamera lengo ni kupata picha zote za vyombo vya usafiri vitakavyokuwa vikiingia na kutoka katika Jiji la Dodoma” alisema Fungo.

Aliongeza kuwa wana mpango wa kuunganisha mfumo huo na taasisi nyingine ili kuimarisha ulinzi na usalama. “Mfumo huu baada ya muda tutauunganisha na taasisi nyingine muhimu kama vile Uhamiaji na NIDA ili kuweza kuwa na muunganiko mmoja wa kufanya kazi, pia kuhakikisha Jiji lote linakuwa salama” aliongeza Fungo.




Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Wisjane Smart Sytem, Wisley Ussiri ambae ni mtekelezaji wa mradi huo alisema kuwa mradi utatekelezwa kwa kipindi cha miezi mitatu na kamera hizo zitafungwa katika barabara kuu nne za Jiji la Dodoma na zile zinazounganisha barabara kubwa. “Tunashukuru kwa kupata tenda hii ya kufunga kamera katika Jiji la Dodoma, naamini tutafanya kazi vile mkataba unavyotaka na kwa muda sahihi uliopangwa. Kwasababu tunafahamu lengo la serikali ni kuhakikisha wananchi na wawekezaji wanaokuja kuwekeza jijini wanakua na uhakika wa usalama wao na mali zao” alisema Ussiri.

Comments

Popular Posts

Osterbay Dodoma wajitokeza usafi wa mazingira

Usafi wa Mazingira Kipaumbele Kata ya Chamwino

Wananchi wa Kata ya Mtumba wanufaika na Mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri