Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma ahimiza matumizi ya mfumo NeST
Na. Nancy Kivuyo, DODOMA
Mkurugenzi
wa Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko aeleza kuwa mfumo wa kielektroniki wa
manunuzi ya Umma NeST katika kufanya manunuzi ya vifaa vya serikali ni mfumo rafiki
unaorahisisha manunuzi na kuweka taarifa hizo katika hali ya usalama.
Aliyazungumza
hayo katika Baraza la Madiwani la kawaida liliofanyika katika ukumbi wa
mikutano wa halmashauri alipokuwa akijibu maswali ya papo kwa papo kutoka kwa
madiwani.
Alisema
kuwa mfumo wa manunuzi wa NeST upo tayari kwa mujibu wa sheria na umeonyesha
matokeo chanya. “Niwajulishe ndugu wajumbe ya kwamba, mfumo huu hatuna namna ya
kuepuka kuutumia kwasababu ndio mfumo ambao tunapaswa kuwa nao ili kufanikisha
manunuzi ya vifaa mbalimbali vya serikali” alisema Dkt. Sagamiko.
Aliongeza
kuwa mfumo haumlazimishi mnunuzi kununua kila kitu kwa wakati mmoja. “Mfumo huu
unahitaji ushirikiano ili uweze kufanya manunuzi yako. Kikubwa ni wewe
kuhakikisha unafahamu unafanya manunuzi ya kiwango gani. Hakikisha unafahamu mradi
utekelezwa kwa ukubwa upi ili iwe rahisi kununua vifaa kwa wakati. Wengi wenu
mnaogopa kufanya manunuzi kwa awamu kwa kuhofia gharama za manunuzi kuwa juu. Niwatoe
hofu, mfumo ni rafiki unaweza hata kununua kifaa kimoja kwa wakati mmoja”
aliongeza Dkt. Sagamiko.
Alimalizia
kwa kusema kuwa watumiaji wa mfumo wa manunuzi wa NeST wawe na desturi ya
kuwasilisha changamoto wanazokutana nazo wakati wa matumizi ya mfumo ili kuweka
mazingira mazuri ya uboreshaji wa mfumo huo. “Rai yangu ni kwamba, tutoe
taarifa za changamoto ili ziwasilishwe na zifanyiwe kazi kwa maboresho zaidi. Tukifanya
hivi mfumo huu utaimarika na kuendelea kutoa huduma nzuri za manunuzi na
kuhakikisha kuwa kuna usiri wa nyaraka za manunuzi tofauti na kipindi cha nyuma
taasisi zilikuwa zikinunua mifumo ambayo kiusalama haikuwa sawa. Waliotengeza mfumo
huu ni vijana wa kitanzania hivyo tutumie vya kwetu” alimalizia Dkt. Sagamiko.
Naye
Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe alisema kuwa rai yake ni kwamba
watu wafuate utaratibu wa manunuzi kwasababu hakuna namna wataepuka matumizi ya
mfumo wa NeST. “Nilihudhuria kikao cha ALAT mkoa na suala la mfumo huu
ulizungumzwa na kila mkurugenzi na rai yao wote ilikua ni kwamba watumiaji wa mfumo
huo wasikae kimya wapatapo changamoto ni vema wakawa na desturi ya kuripoti ili
kufanya marekebisho ili mfumo ukae sawa na kuwa rafiki kwa matumizi. Kwahiyo ninaamini
kila mmoja wetu ana jukumu la kuhakikisha mfumo huo unaimarika” alisema Prof. Mwamfupe.
MWISHO
Comments
Post a Comment