Wananchi waitwa kupima magonjwa yasiyoambukiza bure Nyerere Square

 

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

Mratibu wa Magonjwa Yasiyoambukiza Mkoa wa Dodoma, Dkt. Missana Yango amewataka wananchi jijini Dodoma kujitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi la upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza linaloambatana na utoaji wa elimu ya afya kuhusu magonjwa mbalimbali.

 


Alitoa wito huo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika bustani ya mapumziko Nyerere Square, ambapo maadhimisho hayo ya wiki ya upimaji wa magonjwa yasiyoambukizwa yakiendelea jijini Dodoma.

 

Alisema kuwa huduma hizo zinatolewa bila malipo na zinahusisha upimaji wa magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, saratani, magonjwa ya moyo pamoja na utoaji wa elimu ya lishe bora na mtindo wa maisha wenye afya. “Lengo letu ni kuwafikia wananchi wengi kadri iwezekanavyo, ili wajitambue kiafya na kuchukua hatua mapema kabla magonjwa haya hayajawa sugu. Huduma zote tunazotoa hapa ni bure, hivyo tunawahimiza wananchi wajitokeze kwa wingi” alisema Dkt. Yango.

 

Aliongeza kuwa kampeni hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali kupitia Wizara ya Afya na ofisi ya Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma katika kupambana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza ambayo yamekuwa yakiongezeka kutokana na mabadiliko ya mfumo wa maisha.“ Lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wake wanakuwa salama kiafya pia magonjwa yasiyoambukiza yanaongezeka kwa kasi, hivyo ni muhimu kila mmoja wetu achukue hatua mapema” alisema Dkt. Yango.

 


Nae, Mkazi wa Nzuguni ambae alichangia damu na mnufaika wa matibabu, Tumaini Shauri alipongeza juhudi hizo zinazofanywa na serikali akisema zimekuwa zikiwasaidia kutambua hali zao za afya na kupata ushauri wa kitaalam. “Kwa kweli nashukuru sana serikali kwa kuliona hili na kutuletea huduma hizi bure katika halmashauri ya Jiji la Dodoma. Nilivyosikia tangazo hili nikaona nije nipime magonjwa yote yaliyotangazwa na nimefanikiwa, pia nimepewa ushauri na madaktari, lakini pia niwahamaishe wananchi wenzangu kujitokeza katika zoezi hili kwasababu ni bure” alisema Shauri.

 

Zoezi hilo linatarajiwa kuendelea kwa siku tatu na kuhitimishwa tarehe 14 Novemba, 2025.


 

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

Halmashauri ya Jiji la Dodoma Kuhudumia Majimbo Mawili ya Uchaguzi

Miaka minne ya Dkt. Samia, Kizota yanufaika mikopo ya asilimia 10