Changia Damu kuokoa maisha

 

‎Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

‎Wananchi wahimizwa kuchangia damu ili kuokoa maisha ya wale wanaopata dharura ya kuhitaji huduma ya kuongezewa damu.


‎Hamasa hiyo ilitolewa na Mkuu wa Timu za Ukusanyaji Damu Kanda ya Kati, Dr. Leah Kitundya katika kliniki ya upimaji wa bure wa magonjwa yasiyoambukiza inayoendelea katika bustani ya mapumziko Nyerere Square jijini Dodoma.

‎Alisema kuwa kila mwananchi anawajibu wa kuchangia damu kwasababu inasaidia wakati wa uhitaji. "Wananchi mliopo hapa Nyerere Square tunawaomba na kuwakumbusha kuchangia damu kwasababu itatusaidia sote wakati wa uhitaji. Damu yako inaweza kumsaidia mtu ambae hukutegemea ingemfikia. Changia kuboresha afya za wengine" alisema Dr. Kitundya.

‎Aliwaita wananchi kuchangia damu huku akiwakumbusha kujitokeza kwa wingi kujitolea kwasababu zinapotokea ajali ama dharura za kuhitaji damu kwaajili ya kuokoa maisha wapo pia ndugu na jamaa wa karibu wanaweza kukumbwa na kadhia hiyo.


‎"Ndugu zangu, uhitaji wa damu ni wa kila mmoja wetu, ukiona leo hii hakuna umuhimu wa kuchangia damu kesho ndugu yako anaweza kupata ajali au yupo anajifungua ameishiwa damu ikawa changamoto na majuto kupata msaada wa haraka. Lakini ukichangia unakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuhakikisha wapendwa wako wanapata huduma bora na ya haraka ya kupata damu pale inapohitajika" alisema Dr. Kitundya.

‎Kwa upande wake, Balozi wa Taasisi ya  Magonjwa yasiyoambukiza (NCD), Lawrence Malima ambae pia ni Msanii wa Bongo Fleva aliungana na wataalam wanaotoa elimu kuwasisitiza wananchi kutengeneza utamaduni wa kupima afya ili kugundua maradhi yanayowasumbua huku akichombeza na nyimbo za hamasa. "Kliniki hii ni muhimu kwasababu itawasaidia kufahamu ni magonjwa gani yanawasibu. Lakini hata wale ambao tayari wanaugua watapata huduma za awali hapa na watajua hali zao zinaendeleaje. Nawapongeza sana wananchi wenzangu kwa kuja kupata huduma hizi muhimu. Mnaochangia damu tunawapongeza hili mnalofanya ni jema na la kuigwa" alisema.

‎Nae, Mkazi wa Nzuguni na mchangiaji wa damu, Tumaini Shauri alipongeza ujio wa kliniki za matibabu ya bure mara kwa mara na kuishauri serikali kufanya jambo hilo kuwa endelevu.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

Miaka minne ya Dkt. Samia, Kizota yanufaika mikopo ya asilimia 10

Halmashauri ya Jiji la Dodoma Kuhudumia Majimbo Mawili ya Uchaguzi