TLS yashauriwa kusimamia haki na usawa nchini

Na. Janeth Gerald, DODOMA

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Dotto Biteko amekitaka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na mawakili kusimamia haki na usawa nchini ili kuhakikisha haki inatendeka kwa watu kwa lengo la kuchochea maendeleo.


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Dotto Biteko 


Kauli hiyo aliitoa wakati akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufungua mkutano mkuu wa mwaka wa (TLS) uliofanyika jijini Dodoma.

Dkt. Biteko alisema, TLS wakati inaadhimisha miaka 70 tangu kuanzishwa kwake, wanachama wake wanatakiwa kutafakari mwelekeo wa chama hicho kitaaluma ili kuendana na azma ya serikali ya awamu ya sita ambayo imeweka nia thabiti katika kuhakikisha haki inaonekana ikitendeka.

"Tumieni muda kusema na kusikiliza hoja za watu wanaojua na wasiojua kwa kuwa nchi hii inaendeshwa kwa mujibu wa sheria kuhakikisha kuna hekima mahala pa kazi" alisema Dkt. Biteko.

Aidha, aliwataka wanachama wa TLS kutumia taaluma yao kushiriki kikamilifu katika uchaguzi wa serikali za mitaa nchini baadae mwaka huu pamoja na uchaguzi mkuu utakaofanyika baadae mwakani. Aliwahimiza kuchagua viongozi wenye uwezo wa kuleta maendeleo badala ya kuzingatia tofauti nyingne zinazo watofautisha binadamu.

Akizungumzia uchaguzi ndani ya TLS, Naibu Waziri Mkuu aliwataka wajumbe kuchaguana kwa kuzingatia vigezo, nia na mwelekeo wa wagombea watakao kiwezesha chama hicho kusonga mbele na siyo wale wataotanguliza maslahi binafsi badala ya chama.

Nae, Rais wa TLS, Wakili Harold Sungusia alisema kuwa katika kitabu cha orodha ya mawakili nchini idadi ya mawakili imefikia 12,471. Alisema kuwa ongezeko hilo la mawakili litasaidia kutatua changamoto zilizopo za kisheria. 

Akiongelea tabia ya kukamata kamata mawakili wakati wakitekeleza majukumu yao vimepungua. "Vitendo vya kukamatwa kwa mawakili hadharani wakati wakiwakilisha wateja wao vimepungua sana ikilinganishwa na miaka iliyopita. Tunatamani useme neno Mheshimiwa mgeni rasmi ikiwezekana kwa kuwa ni aibu wakili kushikwa ‘Tanganyika jeki’ akiwa kazini" alisema Wakili Sungusia.

 

Habari hii imehaririwa na Frola Nadoo

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma