Nanenane ni muhimu kujifunza Kilimo na Ufugaji bora

Na. Rahma Abdallah na Jackline Patrick, NANENANE

Maadhimisho ya siku ya wakulima Nanenane ni maonesho ya muhimu ambayo humwezesha mwananchi kujifunza katika kilimo, ufugaji pamoja na uvuvi. Maonesho hayo ni mahususi kwa kila mtanzania katika kuzalisha mazao yenye tija kwa kutumia teknolojia ya kisasa.




Hayo yalizungumzwa na Diwani wa Kata ya Kikombo, Emmanuel Manyono alipokua akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maonesho ya kimataifa ya Nanenane jijini Dodoma.

Manyono alisema kuwa maadhimisho hayo yanaleta tija kwa jamii na pia kuwapa wakulima elimu ya kilimo na ufugaji bora. “Maonesho haya yamekua yakileta tija, kumekua na mafunzo mengi yakisaidia wakulima kuondokana na kilimo cha zamani na sasa kulima kwa kuzingatia kilimo cha kisasa. Kilimo cha kisasa kinamafanikio makubwa, mkulima analima shamba dogo linalotoa mazao mengi na bora. Hivyo, rai yangu wakulima wajifunze kulima kilimo cha kisasa. Wananchi wajitokeze katika maonesho ya Nanenane hapa Nzuguni kujifunza mbinu bora za kilimo cha kisasa na matumizi ya teknolojia za kilimo’’ alisema Manyono.

Pia alisema kuwa kuwepo kwa maonesho hayo kunaleta chachu kwa wakulima nchini kutokana na fursa zinazotolewa kwa wakulima wote katika uuzaji wa mazao kwa kunufaika zaidi na kilimo chao. Tofauti na mfumo wa kizamani ambao ulikua ukiwanyonya wakulima, aliongeza.

Akiongelea changamoto zinazowakabili wakulima, alisema ni uelewa na kufuata maelekezo ya wataalam kuhusu kilimo bora. “Maonesho ya Nanenane yanasaidia utoaji wa elimu kwa sababu wananchi wanaelimishwa huku wakiona kwa macho. Hivyo, maonesho haya yanaleta mabadiliko kwa mtu binafsi na taifa kwa ujumla. Hivyo, nawaomba wananchi wote kujitokeza kwa wingi katika mabanda has abanda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa ajili ya kupata elimu ya kilimo bora’’ alisema Manyono.

Maadhimisho ya kimataifa ya Nanenane kanda ya Kata yalianza tarehe 1-8 Agosti, 2024 yakiongozwa na kaulimbiu isemayo ‘Chagua viongozi bora wa Serikali za Mitaa kwa maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi’.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma