Jiji la Dodoma kinara taaluma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeendelea kufanya vizuri katika taaluma kwa kufaulisha kwa asilimia 93.18 wanafunzi waliohitimu elimu ya msingi mwaka 2023 kutokana na ushirikiano mzuri baina ya halmashauri na wadau wa sekta ya elimu.

Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Prisca Myalla alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za elimu


Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Prisca Myalla alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za elimu katika kikao cha wadau wa elimu kilichofanyika katika Shule ya Msingi St. Gasper iliyopo jijini Dodoma.

Mwl. Myalla alisema “Halmashauri ya Jiji la Dodoma kupitia Divisheni ya Elimu Awali na Msingi imeendelea kufanya vizuri katika taaluma kupitia matokeo ya mitihani mbalimbali ya kuhitimu elimu ya msingi na Mtihani wa Upimaji Darasa la Nne. Aidha, shule binafsi zimeendelea kufanya vizuri kwenye mitihani hiyo na kuchangia ongezeko la wastani wa ufaulu kutoka wastani 179 kwa mwaka 2022 na kufikia wastani wa 189 kwa mwaka 2023. Jumla ya watahiniwa 14,907 sawa na asilimia 93.18 waliohitimu elimu ya msingi 2023 walifanikiwa kufaulu na kujiunga na kidato cha kwanza kwa mwaka 2024. Hatua hii ni ya mafanikio makubwa ukilinganisha na hali ya ufaulu wa mwaka 2022 ambapo asilimia ya ufaulu ilikuwa 89.90”

Kuhusu elimu jumuishi, alisema kuwa halmashauri inatekeleza Elimu Maalum na Jumunishi katika shule 61 zinazopokea wanafunzi wenye mahitaji maalum. “Kati ya shule hizo zenye vitengo ni 11 (Hombolo Bwawani, Mpunguzi, Mlezi, Kisasa, Nala, Chinangali, Nzunguni B, Generali Msuguli, Mbwanga, Nkuhungu na Ndachi) shule maalum moja ya Dodoma Viziwi na shule 50 ni Jumuishi” alisema.

Akiongelea utatuzi wa changamoto ya miundombinu ya madawati na maji katika shule za awali na msingi, alisema kuwa halmashauri inaendelea kuzitafutia ufumbuzi. Halmashauri imetenga shilingi 358,890,000 kutoka mapato ya ndani kwa ajili ya kutengeneza madawati 3,418 katika mkakati wake wa kupunguza changamoto ya upungufu wa madawati kwa wanafunzi wa shule za msingi. Halmashauri imetenga fedha kwa ajili ya gharama za uchimbaji wa visima kwenye maeneo ya shule ili kuweza kupatikana kwa huduma ya maji kwa wanafunzi. Halmashauri inaendelea kulipa madeni ya walimu mbalimbali kama vile likizo, malipo ya wastaafu pamoja na uhamisho kadri fedha zinavyopatikana kutoka serikali kuu au mapato ya ndani” alisema Mwl. Myalla.

Katika kuhakikisha shule zote zinatoa huduma ya chakula shuleni, katika msimu huu wa mvua shule zote zenye maeneo ya kulima zimeagizwa zilime mazao mbalimbali ya chakula kama Mtama. “Halmashauri imetenga bajeti ya shilingi 100,000,000 kwa ajili ya kununua mahindi yatakayoandaliwa na kusagwa ili kugawiwa shuleni kwa ajili ya uji kwa wanafunzi hasa kwa shule zenye matokeo duni ya mitihani mbalimbali” alisema Mwl. Myalla.

Kikao cha wadau wa elimu katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma kilifanyika kwa lengo la kuwapa fursa wadau wa elimu kujadili mafanikio na changamoto za sekta ya elimu na kutoa zawadi kwa shule zilizofanya vizuri, walimu na wanafunzi na viongozi walioshiriki katika kuhamasisha elimu katika Mkoa wa Dodoma.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma