DC Shekimweri ampa Tano Mkurugenzi John Kayombo

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MKUU wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri amemshukuru Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kutoa kipaumbele katika maendeleo ya sekta ya elimu kwa kutoa fedha nyingi katika ujenzi wa miundombinu ya sekta ya elimu.



Alhaj Shekimweri alisema “nitakuwa nimekosa uungwana nisipomshukuru hadharani Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, John Lipesi Kayombo. Tulikuwa na mkutano wa viongozi wakuu wa Wilaya ya Dodoma, Mstahiki Meya, Mbunge, Mkurugenzi wa Jiji na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi mzee Mamba. Akiwa mgeni tukataka tushirikiane nae kwenye dira ya wilaya na tukataka tufahamu vipaumbele vyake kama kijana ambae anataka kuacha alama katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Nataka niwaambie leo hadharani, Kayombo alisema mimi napokea maelekezo na ushauri wenu wote mnaonipatia kama viongozi wangu, lakini la kwangu lililo moyoni mwangu ninatamani niache alama katika sekta ya elimu”.

Alisema kuwa mkurugenzi huyo ametoa fedha nyingi katika ujenzi wa miundombinu ya elimu. “Lakini leo kuna kitu cha ‘surprise’ nimekiona hapa, anakwenda kutambua divisheni kwa jitihada walizozifanya na kuwapatia fedha. Najua ukubwa wa sekta ya elimu msingi na wingi wa shule na wataalamu wanaosimamia, amewapatia shilingi 5,000,000 kutambua jitihada zao kwa kazi wanazozifanya hiki ni kitu kikubwa sana. Lakini ametoa shilingi 3,000,000 kwa upande wa elimu sekondari pia kutambua jitihada zao. Ninaongea na wadau wa elimu na wakuu wa shule na walimu wakuu na waratibu elimu kata, nina dhani mmepata pacha mzuri wa kufanya nae kazi, hebu mumpatie ushirikiano mzuri ninaenda kuiona wilaya yetu ikipaa kielimu kwa ajili ya kazi za huyu mkurugenzi” alisema Alhaj Shekimweri.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma