Dodoma Jiji FC, yawapigia hesabu kali Wanangushi

Na. Mussa Richard, DODOMA

Klabu ya Soka ya Dodoma Jiji FC, hii leo itashuka dimbani kukipiga na klabu ya Soka ya Coastal Union ikiwa ni muendelezo wa mbilinge mbilinge za duru ya lala salama ya ligi kuu ya NBC Tanzania Bara, mchezo utakaochezwa katika dimba la Jamhuri jijini Dodoma, majira ya saa 3 kamili usiku.




Akizungumza wakati wa mkutano kabla ya mchezo, Kocha mkuu wa Dodoma Jiji FC, Meck Mexime aliweka wazi ugumu wa mchezo kuzingatia ligi inaelekea ukingoni. “Ligi inaelekea ukingoni mpaka sasa haijulikani nani anashuka nani anabaki jambo ambalo linafanya kila mchezo kuwa kama fainali. Kila timu tunayokutana nayo inakuwa imejiandaa vizuri lakini sisi hilo halitutishi kwasababu maandalizi yetu ni ya kufanya vizuri kwenye kila mchezo bila kujali ni nani tunaenda kukutana nae, jambo jingine linalofanya mchezo huu kuwa mgumu ni timu zote mbili tumetoka kupoteza michezo yetu iliyopita. Kwahiyo, kila timu inaingia kwenye mchezo huu kutafuta matokeo ili kuweza kutengeneza mazingira mazuri ya kukaa nafasi nzuri kwenye msimamo wa ligi, makosa ya mchezo uliopita tumeyafanyika kazi kwenye uwanja wa mazoezi kesho tunakuja tukiwa na nguvu mpya na ari mpya kuhakikisha alama tatu zizabaki nyumbani” alisema Mexime.

Nae, mchezaji wa Klabu ya Soka ya Dodoma Jiji FC, Abdi Banda akaelezea hali ya kikosi kuelekea kwenye mchezo wa leo dhidi ya Coastal Union. “Kama wachezaji tumejiandaa vizuri kwenda kukabiliana na Coastal Union tunajua mchezo utakuwa mgumu lakini sisi tumejiandaa kwenda kufanya vizuri ili tuzidi kupanda kwenda nafasi za juu zaidi kwenye msimamo wa ligi, makosa ya mchezo uliopita tumeshayafanyia kazi na katika mchezo wa leo tunaamini tutapata matokeo ya ushindi” alisema Banda.



Kwenye msimamo wa ligi kuu ya NBC Tanzania Bara Dodoma Jiji FC, ipo katika nafasi ya saba ikikusanya alama 26, ikishuka dimbani mara 21, ikishinda michezo saba, ikitoka sare michezo mitano, ikipoteza michezo tisa, ikifunga mabao 22, ikiruhusu wavu wake kutikiswa mara 27.

Habari hii imehaririwa na Nancy Kivuyo

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma