Bilioni 9.1 yanufaisha vikundi kwa Mwaka 2020-2023

Na. Faraja Mbise, IPAGALA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma ilitoa takribani ya shilingi bilioni 9.1 kwa ajili ya kuwezesha vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ndani ya kipindi cha Mwaka 2020 hadi 2023.



Hayo yalisemwa na Kaimu Afisa Maendeleo ya Jamii, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Patrick Sebyiga alipofanyiwa mahojiano na waandishi wa habari, mara baada ya kumalizika kwa ziara ya Kamati ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Dodoma kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Jiji la Dodoma.

“Kwa mikopo ya asilimia 10 kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, kuanzia Mwaka 2020 hadi 2023, Halmashauri ya Jiji la Dodoma imetoa kiasi cha shilingi bilioni 9.1 ikiwa na maana vikundi 767 vimepata mkopo. Vikundi vya akina mama 407, vijana 279 na watu wenye ulemavu 81 hii ni sawa na watu 4,883 wamenufaika na mkopo wa asilimia 10” alisema Sebyiga.

Akizungumzia kuhusu faida za mkopo wa asilimia 10, alisema kuwa mkopo huo una faida kubwa sana na unawawezesha kuongeza kipato chao na kuboresha maisha yao kwa ujumla. “Mikopo ya asilimia 10 kwakweli imewasaidia watu wengi, mfano kikundi tulichotembelea leo, umeona ufugaji unaoendelea pale pamoja na wao kuweka nguvu yao na serikali imeweka nguvu pale kwa kiasi walichopata kimewasaidia sana takribani shilingi milioni 20. Hivyo, imewasaidia maisha yao na hata kipato chao kinakua” alisema Sebyiga.

Sambamba na hilo alisema kuwa kuna changamoto katika kufanya marejesho hasa kwa vikundi vya vijana kutokana na kufanya vitu ambavyo ni tofauti na walivyovikusudia kufanya pindi walipoomba mkopo huo. “Wenye changamoto kubwa ya kurudisha mikopo ni vijana, kwasababu wanapochukua hii mikopo muda mwingine wanafanya shughuli ambazo wanakuwa hawajaandika kwenye andiko lao. Natoa ushauri kwamba, wanapochukua hii mikopo basi wafanye kile ambacho wamekipanga” alisema Sebyiga.

Pia alitoa rai kwa wananchi wenye vigezo vya kupata mikopo hiyo kuchangamkia fursa kwasababu mikopo hiyo imeletwa kwa ajili yao. Sebyiga alisema “tunawahamasisha wananchi waende kwenye kata zao watume maombi na waombe, hii pesa ipo kwa ajili yao waweze kupata hii mikopo ili iweze kuwasaidia katika shughuli zao za kimaendeleo”.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma