Wananchi waaswa kujitokeza kwa wingi katika Kliniki ya Ardhi

 Na. Aisha Ibrahim, VIWANDANI

Afisa Maendeleo ya Jamii, Dawati la Msaada wa Kisheria Jiji la Dodoma, Frida Ngowi, amewataka wakazi wa jiji hilo kujitokeza kwa wingi katika Kliniki ya Ardhi inayoendelea kutolewa katika eneo la ilipokuwa Manispaa ya zamani kwa lengo la kupata msaada wa kisheria na kuweza kutambua njia muhimu za kutatua migogoro ya ardhi na kupata haki stahiki.



Dawati hilo liko chini ya Kampeni ya 'Msaada wa Kisheria wa Mama Samia' ijulikanayo kama “Samia Legal Aid Campaign” ambayo inaongozwa na Wizara ya Sheria na Katiba.

Akizungumzia kuhusu msaada wa kisheria alisema kuwa lengo ni kuwasaidia wananchi wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za Mahakama ili kuweza kutatua changamoto mbalimbali za Ardhi zanazohitaji msaada wa kisheria. “Lengo letu ni kutatua changamoto mbalimbali za watu wote wasioweza kupeleka madai yao mahakamani. Hivyo, sisi ni kiungo kati ya Mahakama na wananchi kupatiwa msaada wa sheria” alisema Ngowi.

Aliongeza kuwa, watu wote wana haki ya kupata msaada wa kisheria kwa amani na utulivu wa hali ya juu hivyo wananchi wasisite kujitokeza kwa wingi kuelezea changamoto zao kwasababu katika nchi ya Tanzania hamna mtu yeyote aliye juu ya sheria. “Niwasisitize wananchi mjitokeze kuelezea shida zenu kwasababu ni haki yenu na nchi hii hakuna mtu mkubwa juu ya sheria” alisisitiza Ngowi.

Kwa upande wake, mkazi wa Kata ya Ipagala, Samson Yaledi, alisema kuwa wamekuwa wanakutana na changamoto ya kuzungushwa huku na huku kupata hatimiliki na utambulisho wa viwanja vyao kwa muda mrefu bila kufanikiwa jambo linalowapekelea kukata tamaa kwasababu idara ya Ardhi imekuwa nyuma katika kutatua changamoto za Ardhi kwa wakati. “Kuhusu suala la Ardhi sisi wananchi tunafikia hatua ya kukata tamaa kufuatilia kwasababu wanaohusika na huduma hizi wanatuzungusha sana bila kufanikiwa kwa wakati” alisema Yaledi.

Pia, aliwaasa wananchi kuzingatia sheria na taratibu za Ardhi kwa kuacha tabia ya kuanza ujenzi bila ya kuwa na vibali maalum, kuzingatia mipaka na ramani ya viwanja husika ili kuepuka migogoro isiyo ya lazima katika jamii. “Niwaase wananchi wenzangu kuacha tabia ya kuanza ujenzi bila ya kuwa na vibali kutoka serikalini kwasababu kufanya hivyo ni kusababisha migogoro katika jamii na pia ni uvunjaji wa sheria na taratibu za nchi” alisema Yaledi.

Nae, mkazi wa Kata ya Kilimani, Haruna Kifimbo, aliomba serikali kutafuta njia mbadala ya kuwashirikisha watendaji na wenyeviti wa mitaa kushiriki katika Kliniki ya Ardhi kwasababu wao ndiyo washughulikiaji wa mwanzo wa kero za Ardhi kabla ya kufikisha ngazi za juu. “Mimi kama mwananchi naiomba serikali iwashirikishe hata viongozi wetu wa mitaa na watendaji nao waweze kuwa miongoni mwa kliniki hii kwasababu ndiyo wanaoshughulikia kesi zetu mwanzo kabisa kabla ya kufika juu” alisema Kifimbo.

Aidha, alishauri kuwa ni vema wasimamizi wa kliniki hiyo wangekuwa wanatoka mikoa mingine, nje ya Jiji la Dodoma, kuja kusikiliza malalamiko yao na kuweza kuyatatua kwasababu baadhi ya changamoto zao zinasababishwa na wasimamizi haohao waliowekwa kusimamia kliniki hiyo. “Nitoe ushauri kwa serikali kuleta wasimamizi wa Kliniki ya Ardhi kutoka mikoa mingine mfano Singida na Morogoro ili waweze kuendesha hili zoezi kwasababu hawa waliotuwekea hapa ndiyo wasababishi wakubwa wa migogoro ya Ardhi na changamoto nyingine kama hizo” alishauri Kifimbo.

Kliniki ya Ardhi iliyoandaliwa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma imelenga kutatua changamoto mbalimbali za Ardhi kwa kutoa huduma zifuatazo; umiliki wa ardhi, huduma za mipango miji, upimaji wa Ardhi, huduma za uthamini, vibali vya ujenzi, migogoro ya Ardhi na huduma za maliasili.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma