Maboresho ya elimu yapelekea kuongezeka kwa ufaulu katika Shule za Awali na Msingi Dodoma

Na. Nancy Kivuyo, KIWANJA CHA NDEGE

Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi Halmashauri ya Jiji la Dodoma yafafanua mafanikio ya maboresho ya elimu katika shule za msingi ambayo inafanya ufaulu wa wanafunzi kuongezeka.






Ufafanuzi huo ulitolewa katika Mkutano wa Wadau wa Elimu na Utambulisho wa Mfuko wa Chakula na Lishe Shuleni ikiwa ni sehemu ya kujadili suala la lishe bora kuboreshwa kwa asilimia zote ili taaluma ya wanafunzi ifikie lengo tarajiwa.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Prisca Myalla alisema “tunaishukuru serikali yetu kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kuboresha elimu na kujenga miundombinu mizuri ambayo kwasasa inasaidia utoaji wa elimu kuwa mzuri. Katika suala la lishe, tunashukuru mfuko wa chakula na lishe shuleni kwasababu unasaidia wanafunzi kuhudhuria shuleni hali inayopelekea mahudhurio kuwa juu ukilinganisha na kipindi cha nyuma”.

Akizungumza kuhusu hali ya ufaulu na jumla ya shule zilizopo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, alisema kuwa kuna jumla ya shule 194 ikiwa serikali inamiliki shule 107 shule mbili zikiwa za mchepuo wa kiingereza na shule za binafsi zikiwa 87. Idadi ya wanafunzi ni 112,699, mahitaji ya walimu ni 2,504 waliopo ni 1,993. Hivyo, Halmashauri ya Jiji la Dodoma ina upungufu wa walimu 511.




“Kuna shule zetu kama vile Shule ya Msingi Amani, Shule ya Msingi Kisasa na Shule ya Msingi Mtemi Mazengo zinaongoza kwa ufaulu wa kiwango cha juu kwa shule za serikali katika jiji letu la Dodoma. Ukifuatilia kwa makini, utagundua shule hizi zina hiyo programu ya chakula shuleni. Kwahiyo, wanafunzi wanapata chakula na hiyo inawaongezea utimamu wa kufuatilia masomo bila kukosa. Kwahiyo, tathmini bado inaendelea kufanyika ili kubaini changamoto zilizopo na kuzitatua” alisisitiza Mwl. Myalla.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Wilaya ya Dodoma, Sakina Mbugi aliwapongeza wadau wa elimu, wakuu wa shule na walimu wakuu kwa kufanya kazi nzuri na kuwataka kuendelea kuisadia serikali ili kuhakikisha jamii inapata elimu bora na nzuri.

“Nawapongeza walimu na watumishi kwa kazi nzuri, tunaomba muendelee kuisaidia serikali katika kuisaidia jamii kupata elimu nzuri, kama kuna mapendekezo ya namna ya kuboresha elimu na lishe katika shule zetu za msingi msisite kuyaleta ili tuweze kuijenga Dodoma iliyo imara kitaaluma” alisema Mbugi.




Akizungumza kuhusu utoaji wa lishe shuleni, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Sebastian Pima alizungumza kwa kukishukuru kikao kuwa “lishe ni mnyororo wa kutengeneza afya. Hivyo, ni muhimu kuangalia ni aina gani ya vyakula vinapatikana katika mazingira yetu ili kujua namna ya kuvitumia. Chakula kinamsaidia mtoto kuongeza usikivu, kuwa na afya njema lakini pia inasaidia mtoto kuondokana na njaa. Kwahiyo, ili elimu yetu iendelee kuwa bora na kutufikisha viwango vya juu ni lazima suala la afya na lishe bora lipewe kipaumbele”.

Wadau wa elimu, afya na lishe walijadili umuhimu wa chakula shuleni huku wakiiipa kipaumbele kaulimbiu isemayo ‘Mlo bora, Mustakabali mzuri’ na kusisitiza kuwa chakula chenye lishe shuleni kitamsaidia mtoto kufanya vizuri katika masomo na ufaulu wa wanafunzi utaongezeka kwa asimilia zote.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma