Dakika 5 kila Mkutano wa Baraza la Madiwani kupata dondoo za Afya Dodoma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

Mkutano wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma umetenga dakika tano kwa ajili ya kupata elimu ya masuala mbalimbali ya Afya ili kuwajengea uelewa mpana madiwani.



Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Mkutano wa Baraza la Madiwani, Prof. Davis Mwamfupe baada ya kuwasilishwa taarifa ya umuhimu wa siku ya Afya na Lishe ya Mtaa (SALIKI) katika mkutano wa Maraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Prof. Mwamfupe alisema alipendekeza kuwa kutokana na maelezo mazuri yaliyotolewa na Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kuhusu maana na umuhimu wa siku ya afya na lishe ya mtaa na lishe kwa ujumla kuna haja ya kutenga dakika tano katika kila mkutano wa baraza la madiwani kupata dondoo muhimu za afya.

Awali akielezea maana ya Saliki, Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe, Dkt. Sebastian Pima alisema kuwa Saliki ni siku ya afya na lishe ya mtaa. “Siku hii ni mjumuisho wa huduma zinazofanyika kwenye jamii nia ikiwa ni kutoa elimu ya masuala yanayohusu afya. Mafunzo ya uandaaji chakula kwa kutumia vyakula vinavyopatikana katika maeneo ya jamii husika, utoaji wa chanjo, kuandaa bustani viroba, afya ya uzazi na kukabiliana na ukatili wa kijinsia” alisema Dkt. Pima.

Katika mkutano huo, Katibu, Joseph Fungo alizitaja kata zilizofanya vizuri katika eneo la lishe kuwa ni Chamwino iliyoshika nafasi ya kwanza ikipewa zawadi ya cheti na shilingi 500,000. Kata ya Ipala mshindi wa pili ilipewa cheti na shilingi 300,000 na Kata ya Chihanga mshindi wa tatu ilipata cheti na shilingi 200,000.

Akifafanua alisema kuwa mshindi wa kwanza kigezo ni kufanya Saliki kwa ubora na kufuata mwongozo. “Mshindi wa pili kigezo ni kufanya Saliki kwa mitaa yote na mshindi wa tatu kuboresha huduma za Saliki” alisema Fungo.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma