DC Shekimweri apongeza Kliniki ya Ardhi jijini Dodoma

Na. Aisha Ibrahim, VIWANDANI

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri, ameipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kurejesha tena Kliniki ya Ardhi inayolenga kutatua kero na changamoto mbalimbali za wananchi zinazohusiana na masuala ya Ardhi.


Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri akisisitiza jambo


Pongezi hizo alizitoa wakati wa ufunguzi wa zoezi la Kliniki ya Ardhi lililoanza leo na kuendelea mpaka tarehe 28 Februari, 2025, eneo la Halmashauri ya Manispaa ya zamani, jijini Dodoma.

Akizungumzia kuhusu umuhimu wa kliniki hiyo, Alhaj Shekimweri alisema kuwa ni vema kufanya tathmini ya kero mbalimbali za Ardhi zilizopita na kuzitafutia ufumbuzi kabla ya kusikiliza kero mpya kwasababu itakuwa ni sawa na kufanya kazi bure kuzungumzia kero moja kila wakati. “Ni vema kufanya tathmini ya mazoezi yaliyopita kwasababu pengine kuna mtu zoezi lililopita alikuwepo na hili yupo kwa changamoto ile ile, huenda hajaridhika na huduma au majibu aliyoyapata kliniki iliyopita ndiyo maana yupo tena” alisema Alhaj Shekimweri.

"Wataendelea kuja kama wanaowashughulikia ni miongoni kwa visababishi vya matatizo yao, yaani mtu anayo kero ya miliki pandikizi alafu anayeishughulikia ndiye aliyesababisha kupatikana kwa kero hiyo kwahiyo tegemea kumuona kila kliniki kwa changamoto ile ile lakini pia mnakubaliana kwenda 'site' na baadae inasitishwa kwahiyo jambo lake ni kama litaanza tena upya, hivyo hapa atakuja mara kwa mara” aliongeza.

Sambamba na hilo alisema, ni lazima kuwepo na dawati maalum la kupokea na kusimamia maoni ya wananchi kwa lengo la kukusanya kero na mapendekezo mbalimbali kutoka kwa wananchi kwasababu jambo hilo litaepusha kupunguza msongamano wa kero zinazojirudia kila wakati. “Kuwepo na dawati la kusikiliza na kupokea maoni yetu na ushauri kwasababu tangu nimefika hapa nimepokea maoni mengi na ni mazuri” alisema Alhaj Shekimweri.

Aidha, alikemea kitendo cha wasimamizi wa Ardhi kushindwa kutimiza majukumu yao kwa wakati kwa kusingizia changamoto ya mtandao na aliwataka kuhakikisha tatizo hilo linatatuliwa haraka iwezekanavyo. “Kuna watu hapa wanataka kusoma, kuangalia hiyo migogoro na hatimiliki mitandaoni, nunueni mtandao wa kisasa wa bila nyaya 'Wi-Fi' na muweke bango kubwa sehemu hii lililoandikwa msimbo ili kila mwenye shida ya mtandao aweze kutatua shida hiyoo na kuepuka visingizio” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, aliomba wazee, wajawazito na watu wenye ulemavu kupewa kipaumbele   na kutengewa eneo maalum katika kliniki hiyo. “Wazee, wajawazito na watu wenye ulemavu wapewe kipaumbele katika huduma hii pia watengewe meza maalum, kwahiyo wazee hawa wasiendelee kuomba hisani kwaajili ya kuhudumiwa kwasababu hatupo hapa kufanya biashara” alisema.

Lakini, aliwasisitiza wananchi kuwa na nyaraka zenye uthibitisho wa eneo analolishughulikia kwasababu maneno bila uthibitisho ni mojawapo ya sababu ya kujirudia kwa kero mbalimbali za Ardhi katika kila kliniki. “Hatuwezi kushughulikia mgogoro ambao mtu anaongea tu bila nyaraka au uthibitisho halisi, mara oooh! Niliuziwa na mauziano hayapo, mara nilitapeliwa kiwanja changu na hakuna nyaraka yoyote” alisisitiza Shekimweri.

Alimaliza kwa kushauri kuwa, wananchi wapatiwe elimu ya kutosha kuhusu haki zao na hatimiliki kwa kufuata misingi ya kisheria ili kuondoa migogoro ya Ardhi na kama hatoridhika na maamuzi ya mahakama anayo haki ya kukata rufaa ilimradi haki msingi ipatikane.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma