Diwani Makole asema neno kwa Machinga Dodoma

Na. Shahanazi Subeti, MAKOLE

Diwani wa kata ya Makole, Halmashauri ya Jiji la Dodoma Omary Haji amewapongeza wafanyabiashara wadogo wadogo (Machinga) wa Mkoa wa Dodoma kwa kuwa na umoja na mshikamano katika utendaji wa kazi kwa lengo la kujikwamua kiuchumi.



Aliyasema hayo wakati wa makabidhiano rasmi ya Ofisi ya Viongozi wa Machinga Mkoa wa Dodoma iliyojengwa Kata ya Makole ambayo imegharimu shilingi milioni 56 zikiwa ni jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa Machinga katika taifa.

Haji alisema “nawashukuru sana Machinga wa Mkoa wa Dodoma, wakiongozwa na wenyeviti wao na viongozi wengine kwa kuweza kuungana katika kufanikisha ujenzi wa ofisi hii na kwakuwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweza kuwatambua Machinga wa Dodoma na kuwajengea ofisi katika eneo hili linaweza kuwasaidia na kuwarahisishia shughuli zenu za kibiashara. Kwahiyo, ni wazi kabisa mtalitunza na kulithamini vizuri jengo hili”.

Sambamba na hilo alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa utu na kuthamini wafanyabiashara wadogo wadogo (Machinga) kwa kufanya mapinduzi katika Kata ya Makole. “Kwahiyo, nina imani kabisa mtalienzi vizuri jengo hili na kama mnavyoliona jengo ni la kisasa zaidi na mmewekewa 'furniture' nzuri lakini mmependezeshewa na jengo lenu ni zuri kuliko hata ofisi ya kata” alisema Haji.



Pia aliongezea kwa kuwataka Machinga kuweza kuwa makini na miundombinu ya ofisi ili iendelee kuwa imara zaidi. “Leo tunaikabidhi ofisi hii, ambayo ndani imekamilika kila kitu, sasa ni jukumu lenu kuweza kusimamia vizuri kwa umakini na kuweza kuhakikisha kwamba vitu vyote  vilivyopo hapa vipo salama. Lakini kutunza mazingira ya eneo lenu la kazi kwa kupanda miti, nina imani kabisa kwa umoja wenu hili jengo linaenda kuwa jipya siku zote. Pia muweze kushirikiana na wenzenu ambao wapo hapa, kuwepo kwenu kwenye Kata ya Makole kunaweza kuchangia haswa maendeleo katika soko letu” alisema Haji.

Mkuu wa Divsheni ya Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Charity Sichona, alielezea kuwa ujenzi wa Ofisi ya Machinga Mkoa wa Dodoma Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa agizo kwa serikali kwamba kila mkoa kujenga ofisi kwa ajili ya viongozi wa Machinga kwa lengo la kurahisisha utoaji huduma kwa wafanyabiashara hao. “Kwahiyo, mara ya kwanza alitoa shilingi milioni 10 kwa kila mkoa kwa kuanza ujenzi. Baada ya ile shilingi milioni 10 kukamilisha ujenzi wake, Halmashauri ya Jiji la Dodoma iliongezea shilingi milioni 26.2 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi. Hadi kufikia hatua ya kukamilika kwa jengo hili jumla ya shilingi milioni 56 zimetumika” alisema Sichona.



Pia alimalizia kwa kusema kuna haja ya wafanyabiashara wadogo wadogo kuweza kupata huduma kutoka kwa viongozi wao. “Sasa tuwakibidhi viongozi waweze kutumia ofisi hii kutoa huduma kwa wafanyabiashara wao. Pia shughuli za uzinduzi rasmi zitakuja kufanyiwa na viongozi wakubwa. Lakini sasa hivi tukabidhi kwasababu kumekuwa kuna uhitaji wa wafanyabiashara wadogo wadogo kupata huduma kwa haraka zaidi” alisema Sichona.

Nae Mwenyekiti wa Christian Msumari, alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanya jambo kubwa lenye kuleta tija katika maendeleo ya Machinga ya kuwa na ofisi ya kusemea kero zao. “Kwasababu hapo mwanzo tulikuwa hatuna sehemu yoyote ya kutolea huduma zetu, lakini kwasasa hivi limekuja jambo la kheri na ni jambo zuri la serikali ya awamu ya sita kwa kututambua na kutuheshimisha, kutujengea ofisi zetu na sehemu za kutolea huduma kama viongozi. Mwanzoni tulionekana kama wahuni, ila sasahivi tunaonekana ni wafanyabiashara wadogo wadogo ambao tupo kwenye mpango wa kukua kwenda kuwa wafanyabiashara wakubwa” alisema Msumari.

Aidha, Mwenyekiti wa wafanyabiashara wa matunda katika Soko la Makole, Denis Athumani, aliishukuru serikali kwa kuona mchango wa wafanyabiashara wadogo wadogo katika kuleta maendeleo. “Vilevile, tunamshukuru kwa kutuletea katika eneo letu la kata ya Makole ambapo nasisi tunaungana na wenzetu katika harakati zetu za utafutaji. Kwahiyo, tunashukuru serikali kwa kutambua umuhimu wetu na fursa hii waliyotupa ili mradi mawazo yetu ya pamoja tuungane katika eneo moja kwa lengo la kuyafikisha ndani ya serikali” alisema Athumani.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma