Mnadani yaweka kipaumbele ulinzi na usalama

 

Na. Dennis Gondwe, MNADANI

WAKAZI wa Mtaa wa Mnadani katika Kata ya Mnadani wametakiwa kuweka kipaumbele swala la ulinzi na usalama ili jamii iwe salama katika kipindi cha sherehe za mwisho wa mwaka.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Mnadani, Hema Wawa akisisitiza jambo


Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Mtaa wa Mnadani, Hema Wawa alipokuwa akiwahutubia mamia ya wananchi wa Mtaa wa Mnadani katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika mtaa huo.

Wawa alisema “tunapoelekea katika sherehe za Krismasi na mwaka mpya, niwaombe sana wananchi wangu msiache makazi bila mtu anayebaki nyumbani. Kipindi hicho kina mkesha, unakuta watu wamefunga nyumba wameenda kwenye mkesha, unarudi nyumbani unakutana na kitu ambacho hukutegemea. Tuchukue tahadhari, kama mnaenda kwenye mkesha mjipe ratiba, wengine waende kwenye mkesha na wengine wabaki waende ibada ya asubuhi. Ulinzi unaanzia kwako mwenyewe kujilinda wewe na mali yako. Niwaombe sana tulisimamie hili ili kuepuka changamoto zinazoweza kudhibitiwa”.

Aidha, aliwatakia heri ya Krismas na Mwaka mpya, 2024 wananchi wa Mtaa wa Mnadani. “Mwisho niwashukuru wananchi wangu kwa uvumilivu wenu, kwa kuacha shughuli zenu na kujitokeza kwa wingi kwenye mkutano huu wa hadhara. Niwaombe sana mabalozi, muendelee kuwapa taarifa wananchi wetu, kuna baadhi wanasema hatujaalikwa, wapeni taarifa. Mkutano kama huu wa hadhara tunapokea maoni yenu na ushauri ili twende pamoja, maendeleo hayawezi kuletwa na mtu mmoja. Tukishirikiana kwa pamoja tunajenga mtaa wetu, kata yetu, wilaya yetu na mkoa wetu, lakini tunajenga taifa letu la Tanzania. Na kufanya hivyo, tutakuwa tumemsaidia Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutekeleza miradi mbalimbali. Mwisho nichukue nafasi hii kuwatakia heri ya Krismas na Mwaka mpya 2024” alisema Wawa.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma