Bodaboda ni kazi, epukeni uhalifu

Na. Dennis Gondwe, MNADANI

VIJANA waendesha Pikipiki (bodaboda) katika Kata ya Mnadani wametakiwa kuichukulia kazi ya kuendesha pikipiki kama kazi nyingine na kujiepusha na kujiunga kwenye makundi ya uhalifu.

Picha kutoka mtandaoni


Kauli hiyo ilitolewa na Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Focus Ishika alipokuwa akiongea na wananchi wa Mtaa wa Mnadani katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika mtaa huo.

Mkaguzi Msaidizi Ishika ambae pia ni Polisi Kata ya Mnadani alisema kuwa vijana waendesha bodaboda wanakosa elimu ya umuhimu wa kazi wanayofanya. “Vijana wetu wa bodaboda wanakosa elimu juu ya umuhimu wa kuichukulia kazi ya bodaboda kama kazi nyingine. Wazazi wenye watoto wanaoendesha pikipiki toeni elimu kwa vijana wenu ajira ya udereva pikipiki waichukulie kama yule anayeamka asubuhi na kwenda benki au kwenda kufundisha (mwalimu) wanatakiwa kuifanya kazi hiyo kwa moyo na bidii. Kwa hiyo makosa tunayo sisi. Mwanao anatoka asubuhi na pikipiki hujui anapaki kituo gani, hujui rafiki zake nani, hujui mishemishe zake ni zipi, unakuja kupewa taarifa kuwa mwanao yupo Polisi amekamatwa unakuja juu, mwanangu siyo mwizi unamjua mwanao vizuri kweli??” alihoji Mkaguzi Msaidizi Ishika.

Aidha, aliwashauri wananchi kuwa wanapopewa taarifa za uhalifu dhidi ya watoto wao kuzifanyia kazi. “Mimi niwaombe, tujaribu kupendana unapopewa taarifa juu ya mwanao ifanyie kazi kuliko kukurupuka kukasirika. Hakuna anayemjua mwanao kama walimwengu, na walimwengu ndiyo sisi” aliongeza.

Alishauri mabalozi kuwa na taarifa sahihi za vijiwe vya bodaboda na usajili wake. “Tusaidiane kuvuka huu mwaka salama sisi pamoja na watoto wetu, usimuonee muhari. Kila balozi anawajibu kupita kwenye kila kituo cha bodaboda kuhakikisha anakikagua, anawajua vizuri waendesha bodaboda na vituo vimesajiliwa. Utaratibu sio mgumu wa kusajili kituo cha bodaboda, unachukua barua kwa Afisa Mtendaji unaenda Latra kituo kinapewa jina na kusajiliwa na idadi inajulikana ni watu 15” alisisitiza.

Vilevile, alishauri kaya kuwa na filimbi kwa ajili ya usalama wao. “Mzee mwenzangu huna filimbi? kuwa na filimbi ili linapotokea piga filimbi watu watoke watoe msaada. Nikisema wangapi wanafilimbi nyumbani kwao hapa nitapata wachache. Kuwa na filimbi na tochi nyumbani kwako kwa ajili ya ulinzi wako binafsi. Mfano, ukiwa na tochi, umesikia kishindo nje, mulika atakimbia tu hakuna mwizi anaependa mwanga, lazima atakimbia tu” alishauri.

MWISHO 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma