Afisa Mifugo Kata ya Mnadani anaupiga mwingi

Na. Dennis Gondwe, MNADANI

KATA ya Mnadani inajivunia utendaji kazi wa Afisa Mifugo kwa kuhakikisha wananchi wanakuwa na mifugo yenye afya kutokana na kupata huduma zote za chanjo kwa wakati.

Afisa Mifugo Kata ya Mnadani, Elizabeth Shirima


Kauli hiyo ilitolewa na Afisa Mtendaji Kata ya Mnadani, Caroline Massawe alipokuwa akitoa taarifa ya mafanikio ya Kata ya Mnadani kwa kipindi cha miaka mitatu (2021-2023) katika mkutano wa hadhara wa wananchi wa Mtaa wa Mnadani.

Massawe alisema “nikiwa Afisa Mtendaji wa Kata ya Mnadani, napenda kumpongeza Afisa Mifugo wa Kaya ya Mnadani, anajitahidi kwa kweli kutekeleza majukumu yake ya kazi anajituma na ni muwajibikaji mzuri sana. Kwa wale wanaofuga natumaini wanalitambua hilo, anawatembelea wananchi kuchanja mifugo yao kwa wakati na mbwa wanaozurura anawachanja pamoja na majukumu mengine, mama huyu anaupiga mwingi”.

Akiongelea mafanikio ya sekta ya mifugo, alisema kuwa sekta hiyo imefanikiwa kudhibiti magonjwa ya mlipuko na magonjwa mengine yanayosababishwa na kupe kwa kutoa elimu kwa wafugaji. “Chanjo mbalimbali za mifugo kama homa ya mapafu kwa ng’ombe, kichaa cha mbwa, kuku pia kuhamasisha wafugaji kuunda vikundi vya wafugaji ng’ombe na kuku. Jumla ya vikundi 11 viliundwa na kupata mikopo kutoka Halmashauri ya Jiji. Vikundi vya ufugaji ng’ombe wa maziwa vitano, vikundi vya ufugaji kuku wa mayai viwili na vikundi vya ufugaji kuku wa nyama vinne” alisema Massawe.

Alisema kuwa kata imefanikiwa kuendesha zoezi la utambuzi wa mifugo na kutoa elimu na kuhamasisha ufugaji bora. “Jumla ya ng’ombe 304 na mbuzi 132 waliweza kutambuliwa na kuvishwa hereni za utambuzi. Elimu ya ufugaji bora wa mifugo hasa ndani ya mabanda, uogeshaji mifugo, uhifadhi wa malisho, matumizi ya vyakula vya ziada na ufugaji wanyama wadogo kama sungura ilitolewa kwa wafugaji” alisema Massawe.

MWISHO


Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma