Wananchi wahamasishwa kujitokeza kuapata huduma Kanda ya Viwandani, Dodoma

Na. Veronica John, DODOMA  

Mkuu wa Kanda ya utoaji huduma ya Viwandani katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Lucas Nkelege amewataka maafisa waliopangwa katika kanda hiyo kuhamasisha wananchi wote wanaojitokeza kupata huduma wanapatiwa huduma kwa viwango vya juu ili waweze kujivunia utendaji kazi wa wafanyakazi hao wa serikali.



Kauli hiyo aliitoa alipokuwa akiongea na wafanyakazi waliopangwa katika kanda hiyo na viongozi wa serikali za mitaa katika kuitambulisha kanda ya utoaji huduma ya Viwandani iliyopo katika jengo la Soko la wazi la Machinga, eneo la Bahi road jijini Dodoma.

Alisema kuwa moja ya jambo muhimu ni kuhakikisha wananchi wa kata zote wanapata huduma kwa urahisi. “Katika kanda hii ya Viwandani, tuna kata saba ambazo tutazihudumia. Hivyo, nitumie nafasi hii kuwasisitiza tu utoaji huduma bora na za viwango ili wananchi wafurahie utumishi wetu. Huduma zote zitatolewa hapa, ila nisisitize zaidi eneo la utoaji wa leseni za biashara na ushuru wa huduma. Nimeamua kutaja huduma hizi mbili ambazo ilikuwa lazima kuzifuata ofisi kuu ya halmashauri. Kwa mapenzi mema ya serikali kwa wananchi wake ikaona iwasogezee huduma kwa ukaribu katika maeneo yenu” alisema Nkelege.

Kwa upande wake Afisa Biashara wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Evodius Nkyabonaki alisema kuwa kupitia kikao hicho alitoa elimu ya masuala ya biashara na uendeshaji wake. “Kupitia kikao hiki pia tumepata nafasi ya kutoa mafunzo na elimu kwa maafisa na viongozi wa serikali za mitaa jinsi malipo ya leseni za biashara pamoja na ushuru wa huduma unavyotolewa na gharama ambazo kila aina ya biashara inapaswa kulipiwa. Hivyo, niwasisitize na maafisa wote kwenda katika kata zao na mitaa yao kutoa elimu hii kwa wananchi wote wanaojishughulisha na biashara. Pia, nawakumbusha maafisa watendaji wote wa kata na mitaa wawe wanapita kwenye mitaa yao na kufanya ukaguzi kuhakikisha wafanyabiashara wana leseni za biashara kwa mujibu wa sheria” alisema Nkyabonaki.



Alisema kuwa wafanyabiashara wanatakiwa kuwa na vitambulisho ambavyo watavitumia kufanya maombi ya leseni za biashara. Pia alitoa rai kwa wafanyabiashara wote katika kanda hiyo kufika katika ofisi ya kanda ya huduma kwa ajili ya kukata leseni ya biashara.

Kwa upande wake, Afisa Afya wa Kata ya Kilimani, Loveness Lyimo alisema kuwa kupitia kikao hicho wamejifunza vitu vingi kutoka kwa afisa biashara na kuwahamasisha wananchi kujitokeza kupata huduma katika Kanda ya Viwandani. “Kwa kweli tunaishukuru sana Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kusogeza huduma hizi karibu zaidi na wananchi kwasababu hapo awali wananchi wakihitaji huduma ilikuwa lazima waende hadi ofisi kuu ya jiji. Lakini kwa kupitia kanda tunaweza kupata huduma kwa urahisi tofauti na awali” alisema Lyimo.

Kanda ya utoaji huduma ya Viwandani inahudumia kata saba ambazo ni Viwandani, Majengo, Makole, Kilimani, Hazina, Uhuru pamoja na Madukani.




MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo