Dkt. Mpango atoa pongezi maandalizi ya Nanenane

Na. Tutindaga Nkwindi, DODOMA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango atoa pongezi kwa maboresho katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi katika maonesho ya kitaifa ya Nanenane kwa kuongeza matumizi ya teknolojia ya kisasa.



Alitoa pongezi hizo wakati wa ufunguzi rasmi wa maonesho ya 32 ya wakulima Nanenane yaliyofanyika katika viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Dkt. Mpango alieleza kuwa serikali imefanya maboresho makubwa yanayoonekana katika sekta hizo, ikiwemo kuimarisha uhifadhi wa mazao ya wakulima, utoaji wa chanjo kwa mifugo, na utambuzi wa mifugo kwa kutumia teknolojia ya kisasa.

Aidha, alisisitiza dhamira ya serikali kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha chakula barani Afrika kwa kuweka mkazo kwenye uzalishaji wa mazao ya kimkakati yenye thamani kubwa ili kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi. “Viongozi wote katika ngazi mbalimbali wanapaswa kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sera za kilimo na kuwahimiza wananchi kutumia ardhi kwa tija, hususani kulima mazao yanayostahimili ukame” alisisitiza Dkt. Mpango.

Alisema kuwa maonesho ya Nanenane ni kiashiria cha uwezo wa sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi kuwa na upatikanaji wa chakula cha kutosha. “Ndugu wananchi, sekta ya kilimo imeendelea kufanya vizuri sana na inaashiria upatikanaji wa chakula ni toshelevu. Wataalam waendelee kutusaidia kutoa elimu ya kutosha na kufanya tafiti yakinifu katika kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wananchi” alisema Dkt. Mpango.



Maonesho ya Nanenane hutoa fursa kwa wakulima, wafugaji, na wavuvi kutoka maeneo mbalimbali nchini kuonesha ubunifu, teknolojia, na mafanikio waliyopata katika sekta zao. Kaulimbiu ya mwaka huu ni “chagua viongozi bora kwa maendeleo endelevu ya kilimo, mifugo na uvuvi, 2025.

MWISHO

Imehaririwa na Nancy Kivuyo

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Vijana waalikwa kushiriki Kongamano S/M Mbwanga