Maziwa ya Mama ni kinga kamili kwa Mtoto

 Na. Leah Mabalwe, DODOMA

Wazazi wametakiwa kuhakikisha wanawanyonyesha watoto wao maziwa ya mama kwa kipindi kinachopaswa ili kuwajengea afya bora na kusaidia ukuwaji wa akili zao, hasa katika miaka ya awali.



Wito huo ulitolewa na Afisa Lishe wa Jiji la Dodoma, Alfa Fanuel wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Maziwa ya Mama Duniani, yanayofanyika kuanzia tarehe 1-7 Agosti, 2025 uliofanyika katika Kituo cha Afya Ilazo, katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Alisema kuwa unyonyeshaji wa maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya mwanzo ni msingi muhimu wa afya ya mtoto, na huchangia kwa kiasi kikubwa katika ukuwaji wa ubongo na kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali. “Utafiti unaonesha kuwa watoto wanaonyonyeshwa ipasavyo huwa na uwezo mzuri wa kiakili, kuwa na kinga thabiti ya mwili, huwa na nafasi kubwa ya kuepuka utapiamlo na maradhi ya mara kwa mara” alisema Fanuel.

Aidha, alihimiza jamii kuondoa mila na desturi zinazokatisha unyonyeshaji wa maziwa ya mama kwa mtoto. “Wajibu wa baba pamoja na jamii kwa ujumla kuwapa wanawake msaada wa kihisia na kimazingira ili waweze kunyonyesha kwa ufanisi, na kuepukana na mila potofu kuhusu kumnyonyesha mtoto” alisema Fanuel.



Kwa upande wake mwananchi wa Kata ya Nzuguni, Amina Juma alitoa wito kwa akina mama kuhakikisha wanawanyonyesha watoto wao kwa kipindi kilichopendekezwa na wataalamu wa afya na kuwapongeza watumishi wa Kituo cha Afya Ilazo kwa kuwapatia elimu hiyo. “Ni wajibu wa kila mama kuhakikisha mtoto ananyonyeshwa kwa miezi sita ya mwanzo bila kupewa chakula kingine chochote. Hii ni kinga ya asili inayosaidia mtoto kuwa mwenye afya bora na akili kwa ujumla na niwapongeze watumishi kwa kutupatia elimu hii na sisi tutakuwa wajumbe wazuri kwa kuwaelimisha akina mama wengine” alisema Juma.

Maadhimisho hayo yameambatana na elimu kwa wazazi kuhusu lishe bora, unyonyeshaji na umuhimu wa huduma za afya za mara kwa mara kwa watoto wachanga.

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo

IAA Tawi la Dodoma kuendelea kulea wataalam kwa vitendo