Kanda Namba Tatu yajifagilia utoaji huduma bora kwa mteja

Na. mwandishi Wetu, KIZOTA

Kanda Namba Tatu katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaadhimisha Wiki ya Huduma kwa Mteja kwa kuhakikisha huduma muhimu kwa wananchi na wafanyabiashara zinapatikana muda wote na kwa wakati.



Huduma muhimu zinazotolewa ni pamoja na ukataji wa leseni ya biashara, malipo ya ushuru, malipo ya kodi za majengo, huduma ya elimu ya msingi na sekondari, huduma za ustawi wa jamii, usajili wa vikundi na asasi za kiraia, vibali vya ujenzi, vibali vya sherehe, upatikanaji wa hati na ushuru wa mabango.

Meneja wa Kanda Namba Tatu, Fanuel Lawrence, alisema kuwa muitikio wa wananchi ni mkubwa na umeonesha dhamira ya wazi ya wananchi kupata huduma stahiki. “Wiki ya Huduma kwa Mteja ni muhimu sana kwetu, inatuonesha namna tunavyowahudumia wananchi na mapokeo ya huduma walizopata. Pia inatupa mwanga wa kuboresha zaidi huduma zetu. Kwa ujumla tunafanya kazi kwa weledi na kwa kuzingatia utaratibu lakini katika yote hayo tunatanguliza huduma bora kwa wateja wetu” alisema Lawrence.

Nae, Afisa Biashara katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Steven Maufi, alisema kuwa maadhimisho hayo ni ukumbusho kwa watumishi kutoa huduma bora na kujenga mahusiano mazuri na wananchi. “Huduma nzuri huleta furaha na mshikamano. Niwahimize watumishi wenzangu kuzingatia lugha za staha, kusikiliza kwa makini wateja na kutoa maamuzi yenye busara kwa mustakabali wa pande zote mbili yaani kwa mteja na halmashauri” alisema.

Kwa upande wake mkazi wa Kata ya Kizota, James Wamalya alieleza kuridhishwa na uwepo wa ofisi hizo karibu na maeneo yao. “Tunashukuru sana ofisi hizi za kanda kuletwa karibu. Zimetusaidia kuokoa muda mwingi na gharama za kufuata huduma mjini. Hongera kwa halmashauri kwa kutujali sisi wananchi” alieleza.

Maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa Mteja yanathibitisha dhamira ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, haraka na kwa ukaribu.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Kanda Namba Mbili yaendelea kutoa huduma bora kwa wananchi

Kanda Namba Mbili yang'ara kwa huduma bora kwa wateja